Na mwandishi wetu
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amezitaka
halmashauri zote nchini ziendelee kutekeleza agizo la Serikali la kutenga
maeneo rafiki yatakayowawezesha vijana kushiriki shughuli za uzalishaji mali
ili kuwaepusha na kero ya kufanya biashara kwenye maeneo hatarishi.
Ametoa agizo hilo (Jumatano, Oktoba 12,
2022) alipozindua Maadhimisho ya Wiki ya Vijana Kitaifa yanayofanyika katika
viwanja vya Gymkhana mkoani Kagera. “Maeneo haya ni lazima yawe na sifa
zinazoendana na shughuli zinazofanywa na vijana”.
Pia, Waziri Mkuu amemuagiza Waziri wa
Nchi - Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Profesa
Joyce Ndalichako ashirikiane na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Angela
Kairuki ili kuhakikisha agizo hilo linatekelezwa ipasavyo.
Mbali na agizo hilo, Mheshimiwa Majaliwa
amewaasa vijana kutumia vizuri fursa zilizopo nchini katika kujiletea maendeleo
na kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana, ambayo inayoikabili
dunia kwa sasa.
Waziri Mkuu ameongeza kuwa fursa
nyingine kwa vijana ni uhusiano mwema wa kidiplomasia na nchi zote duniani.
“Fursa hii ikitumiwa vizuri na kundi la vijana wataweza kunufaika na kusonga
mbele kimaendeleo”.
Akizungumzia kuhusu suala la mitaji,
Waziri Mkuu amesema kuna mifuko mingi ya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi,
hivyo waitumie ili kupata mikopo hususan mikopo itokanayo na mapato ya ndani ya
Halmashauri na kuwekeza katika miradi yenye tija.
Kadhalika, Waziri Mkuu amewasihi vijana
wawe wazalendo na walinzi wa miundombinu ya miradi ya maendeleo inayotekelezwa
na Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. “Wakati
Serikali inaboresha miundombinu ya kiuchumi, uendelevu wake unategemea sana
uzalendo na hali ya kujitegemea kwa Watanzania.”
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili
wa Rais Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi, Hamza Hassan Juma amesema
maadhimisho ya Wiki ya Vijana Kitaifa yanatoa fursa kwa vijana kukutana,
kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu mbalimbali za uzalishaji mali na
uzalendo.
Naye, Waziri wa Nchi - Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na
Wenye Ulemavu, Profesa Joyce Ndalichako amesema Wiki ya Vijana kwa mwaka huu
imelenga kuhamasisha ushiriki wa vijana katika kuleta maendeleo endelevu.
“Vijana wanapaswa kutafakari kikamilifu ushiriki wao katika ujenzi wa uchumi wa
Taifa hasa kipindi hichi ambacho Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan
amefungua fursa za kiuchumi na vijana wakiwa wanufaika wakuu.”
0 Maoni