AFISI YA RAIS, KAZI, UCHUMI NA UWEKEZAJI - ZANZIBAR.

TAARIFA KWA UMMA 07/10/2022.

Hivi karibuni kumekuwa na Taarifa zinazosambaa kwenye Vyombo vya Habari ikiwemo Mitandao ya Kijamii zinazohusiana na kuvunjwa kwa Mkataba wa Ardhi uliotolewa kwa Kampuni ya Pennyroyal Limited inayoendesha Mradi wa Blue Amber uliopo Matemwe Mkoa wa Kaskazini Unguja. Mradi huu wa Uwekezaji ulisajiliwa na Mamlaka ya Kukuza na Kulinda Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), chini ya Sheria ya Mamlaka ya Kukuza na Kulinda Uwekezaji Zanzibar, Sheria Namb. 14, 2018 pamoja na marekebisho yake.

Taarifa hizo pamoja na mambo mengine zinadai kuwa, ufutwaji wa Ardhi hiyo haukuzingatia Masharti ya Kisheria na kwamba, mwekezaji huyo alipata Taarifa kuhusu Suala hilo baada ya ombi lake la kuhuisha Kibali cha Ujenzi kukataliwa na ZIPA. Taarifa hizo hazina ukweli na kwamba, watoaji wa Taarifa hizo wanalengo la kupotosha umma na kuzorotesha Juhudi za Serikali katika Uwekezaji.

Serikali imekuwa na uvumilivu mkubwa juu ya Mradi huu hasa ukizingatia Kasi Ndogo ya Utekelezi wa Mradi  huu kwa kulinganisha na muda tokea ulipoanza. Aidha, Serikali imesamehe takriban Shilingi za Kitanzania milioni 354 za kodi zilizotokana na uingizwaji wa vifaa mbali mbali vya mradi. Haya yote yamefanyika kwa ajili ya kuwezesha na kuwepesisha Utekelezaji wa Mradi huu.

Tunapenda umma ufahamu kuwa, uamuzi uliofikiwa na Serikali ya kufutwa kwa Sehemu ya Ardhi ya Uwekezaji iliyotolewa kwa Kampuni ya Pennyroyal Limited ilitokana na maamuzi halali ya Mahkama yaliyotolewa kwenye Kesi ya Madai Nambari 05/2013 iliyohusisha sehemu ya Ardhi iliyotolewa kwa mwekezaji huyo. kati ya hekta 411.92 alizopewa mwekezaji tokea mwaka 2015 ni hekta ishirini (20) tu ambazo ni chini ya asilimia tano (5%) ndizo zilitumika na ndizo zilizoingia katika kadhia hii na sio eneo lote alilopewa Mwekezaji.

Kufuatia mgogoro uliojitokeza kwa hekta hizo 20, Mahkama iliamuru hekta hizo apatiwe muhusika aliyewasilisha madai yake katika Mahkama. Hata hivyo, Mwekezaji huyo aliamua kufanya ujenzi katika eneo la hekta 20 ambalo lilikuwa na mgogoro kati yake na mdai.

Ni matarajio yetu kuwa Mwekezaji angeheshimu maamuzi ya Mahkama na kutii sheria kama ilivyofanyika kwa upande wa Serikali.

Aidha, katika hatua za kutekeleza Maamuzi ya Mahkama, Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi ilifuta Mkataba wa Ukodishaji Ardhi ya Uwekezaji uliyotolewa kwa mradi huo kupitia Barua yenye Kumbukumbu Nambari CHD.167/173/02/49 ya tarehe 7 Januari 2022, ili kuwezesha Serikali kupima upya eneo lililobaki na kutoa Mkataba mpya wa Ardhi ya Uwekezaji kwa Kampuni hiyo.

Hata hivyo, kabla ya utekelezaji wa maamuzi hayo, Serikali kupitia Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi iliijuilisha Kampuni ya Pennyroyal kuhusiana na dhamira ya kutekeleza maamuzi hayo kwa Barua yenye Kumbukumbu Namba AB.81/167/01/41 ya tarehe 15 Octoba, 2021 hivyo, mwekezaji huyu alikuwa na Taarifa  zote zinazohusiana na suala hili.

Serikali kwa kutambua umuhimu wa uwekezaji nchini ilichukua juhudi mbali mbali za kufanya mawasiliano na mwekezaji huyo kwa lengo la kufanya naye mazungumzo kwa nia ya kutafuta ufumbuzi wa kadhia hiyo. Juhudi hizo za Serikali zilifanyika ikiwa ni ishara ya kuthamini uwekezaji uliowekezwa na kuonesha kuwa Serikali iko tayari kutafuta suluhu ya kadhia hiyo.

Pamoja na juhudi hizo za Serikali, bado mwekezaji huyo alikataa kukutana na Serikali na badala yake kukimbilia kwenye Vyombo vya Habari, jambo ambalo limetushangaza kwa kuzingatia kuwa mwekezaji huyo anatambua kuwa maamuzi yaliyotolewa na Serikali yalitokana na Maamuzi ya Mahkama kwa sehemu tu ya eneo alilopewa kwa uwekezaji na sio ardhi yote.

Hatua iliyofikiwa na mwekezaji huyo imezidisha hofu na mashaka kwa Serikali dhidi wa uwekezaji wake, hasa kwa kuzingatia kuwa mwekezaji huyo ameshindwa kufanya uwekezaji kulingana na mpango wake wa biashara ulioidhinishwa kwa miaka minane (8) sasa tangu Mradi huo uliposajiliwa na ZIPA licha  ya vivutio na fursa za  uwezeshaji alizopatiwa na Serikali katika  kuhakikisha kuwa anafanikisha uwekezaji wake.

Tunapenda kuwatoa wasiwasi wawekezaji wote na kuwahakikishia kuwa, Zanzibar ni sehemu salama na kwamba, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano Tanzania zinathamini mchango wa wawekezaji. Aidha, Serikali zote mbili zimeweka kipamumbele katika kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini na kwa hali yoyote ile Serikali haiko tayari kuona juhudi hizo za Serikali zinazimwa na wawekezaji wachache walioshindwa kutekeleza wajibu wao. Sambamba na hayo, Serikali daima italinda na kusimamia Uhuru na Maamuzi halali yanayotolewa na Mahkama pamoja na kuhakikisha maslab hi ya wawekezaji yanalindwa.                               

Ahsanteni.