Na mwandishi wetu
Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya Zanzibar
Dkt. Salim Slim amesema ni vyema jamii kuweka mfumo madhubuti wa kufanya
mazoezi ili kujikinga na maradhi mbalimbali ikiwemo magonjwa ya Afya ya Akili.
Ushauri huo ameutoa Kinazini mara baada ya kumaliza matembezi
maalum ya kuunga mkono siku ya Afya ya Akili Duniani yanayofanyika kila mwaka
ifikapo oktoba 10 ikiwa ni shamrashamra kuelekea siku hiyo.
Amesema kuwa ili mtu awe na Afya nzuri lazima
awe na mfumo mzuri wa kufanya mazoezi kwani bila ya kufanya hivyo,mfumo wa damu
utakua mzito na kupelekea kupata madhara ya kupoteza kumbukumbu.
“Ikiwa hatufanyi mazoezi katika maisha yetu
angalau kwa dakika 20 kwa kila siku damu itaganda na kuweza kushindwa kufanya
kazi vizuri baada ya hapo kinachofuata ni maradhi kutokana na kuganda kwa damu
katika miili yetu”,alisema Dkt Slim.
Aidha amefahamisha kuwa mfumo wa kufanya kazi
kwa kujiacha unaathiri mwenendo wa afya katika jamii,hivyo kila mtu aangalie
hali ya maisha kwa kufanya mazoezi kwa mujibu wa hali ya Afya aliyonayo.
Nae Daktari dhamana wa Kitengo cha Magonjwa ya
Akili Hospitali ya Kidongochekundu Khadija Abdulrahman amesema kuwa mazoezi
yana uhusiano mkubwa na afya ya Akili katika maisha ya kila siku.
Amefahamisha kuwa watu wengi katika jamii hasa
wafanyakazi hukaa muda mrefu bila kufanya mazoezi, kati yao wanakua na msongo
wa mawazo hivyo kufanya mazoezi kutawasaidia kuondosha vichochezi vya magonjwa
ya Akili na mengine ikiwemo kisukari na shindikizo la damu.
Nao wadau wa Afya kutoka Umoja wa
Mataifa (UN) wamesema kuwa wameamua kufanya hivyo ili kuhamasisha jamii
kushiriki katika kufanya mazoezi ili kuimarisha Afya ya Akili na kujikinga na
maradhi mbalimbali.
Aidha wamefahamisha kuwa kwa mujibu wa Shirika
la Afya Duniani mtu mmoja kati ya
wanne Ulimwenguni kote anaishi na tatizo la
Afya ya Akili , hivyo ni wajibu wakila mmoja kufanya mazoezi ili
kujiepusha na tatizo hilo.
Matembezi ya kilo mita
tano yaliyoambatana na mazoezi ya viungo na upimaji wa Afya yameandaliwa
na wadau wa Afya Zanzibar ikiwemo WHO, UNICEF na UNDP ambapo matembezi hayo
yameanzia Kinazini kuelekea Malindi Vuga,Mnzimmoja Michenzani na kurejea
Kinazini.
0 Maoni