Na
Mwandishi Wetu
Naibu Wakili Mkuu wa
Serikali Dkt. Boniphace Luhende amewataka wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi
ya Wakili Mkuu wa Serikali (OWMS) kutumia mafunzo wanayopatiwa kujenga uelewa
kuhusu umuhimu wa Baraza la wafanyakazi katika kuweka mahala pa kazi kuwa sehemu
salama katika utendaji wa kazi na kuhakikisha kuwa wajumbe wa OWMS wanatekeleza
majukumu waliyokasimiwa.
Dkt. Luhende
ameyasema hayo leo wakati akifungua mafunzo ya siku moja kwa wajumbe wapya wa
Baraza la Wafanyakazi wa OWMS yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Takwimu jijini
Dodoma ambapo amesema kuwa mada tatu zitawasilishwa kwa wajumbe hao ikiwemo Wajibu
na Majukumu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi; Kupitia Mkataba wa Baraza la
Wafanyakazi; na Umuhimu wa Baraza la wafanyakazi mahala pa kazi.
Amewataka wajumbe
kutumia fursa hiyo kuzijua hadidu za rejea ambazo zitawaongoza katika utendaji
kazi wa kila siku na kutekeleza majukumu katika kipindi chote cha miaka mitatu watakachokuwa
wajumbe wa Baraza hilo kuwa nguzo kati ya
Baraza na watumishi wengine kwa kuwa Baraza la wafanyakazi ni chombo muhimu mahala
pa kazi na kuwa sehemu salama ili kuleta tija katika utendaji kazi wa kila siku
wa OWMS na amewataka wajiandae kuhamia Dodoma mwaka huu.
Akitoa mada ya
Umuhimu wa Baraza la Wafanyakazi, Katibu wa TUGHE Mkoa wa Dodoma, Samuel
Nyungwa amesema kuwa ni muhimu kwa kila mtumishi kujiunga na chama cha
wafanyakazi kwa sababu ni taasisi pekee ya wafanyakazi ambayo imeundwa kwa
ajili ya kulinda na kutetea haki kwa kuweka sawa mahusiano ya kazi kati mfanyakazi
na mwajiri wake mahali pa kazi.
Naye Mkurugenzi
Msaidizi wa Rasilimali Watu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia,
Sebastian Innosh amewasilisha mada kuhusu umuhimu na uendeshaji wenye tija wa
mabaraza la wafanyakazi ambapo amesema kuwa mabaraza yanatakiwa kushauri na
kujadili masuala muhimu ya taasisi; kutumia rasilimali watu na fedha kwa
manufaa na uendelevu wa taasisi husika na taifa kwa ujumla; na kuimarisha
mahusiano mema na kudumisha amani na utulivu mahala pa kazi.
Akizungumza kwenye
mkutano huo, Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa, Rugemarila Rutatina amesema kuwa mkataba
wa Baraza la Wafanyakazi unaleta mafanikio na ushirikiano mahala pa kazi kwa
kuwa unawaweka pamoja na kuwaleta karibu watumishi mahali pa kazi.
0 Maoni