Pongezi hizo zimetolewa
jana na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Sumbawanga Rainer Lukala
wakati akiongea na wanufaike wa mikopo katika vijiji vya Msila na Ilemba ikiwa
ni ziara ya ukaguzi wa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
“Maelekezo ya Ilani ya
CCM ni kutumia fedha asilimia kumi ya mapato ya ndani ya halmashauri kwa ajili
ya kuwezesha mikopo kwa makundi ya wanawake, vijana na walemavu kwa riba nafuu.
Tunawapongeza halmashauri kwa kufanikisha hilo” alisema Lukala.
Halmashauri hiyo katika
mwaka 2021/22 imetoa mikopo ya shilingi Milioni Sita (6) kwa kikundi cha
wanawake wa kijiji cha Msila na shilingi Milioni Tano (5) kwa walemavu wawili
wa kijiji cha Ilemba.
Lukala alitoa wito kwa
wanufaike wa mikopo hiyo kuwa na utaratibu wa kuutunza fedha kwenye akaunti za
benki ili wawe na uhakika wa kufanya marejesho na kuwa halmashauri itoe
kipaumbele kwa vikundi vinavyorejesha vizuri ili wapate mikopo awamu ya pili.
Naye Katibu wa Kikundi
cha Kilimo Kwanza kijiji cha Msila kata ya Mfinga Anastazia Joseph alisema
anaomba halmashauri iongeze kipindi cha kurejesha mkopo toka mwaka mmoja hadi
miwili kwa kuwa rejesho la shilingi 500,000 kila mwezi kati ya mkopo wa
shilingi Milioni 6 ni kubwa.
Kikundi hicho chenye
wanachama kumi na mbili (12) kinajishughulisha na kazi za kilimo ambapo
wamelima hekari nne za mahindi na moja ya alizeti huku wanachama wakiweka akiba
na kukopeshana.
Kwa upande wake Joseph
Mwendapole mnufaika wa mikopo ya walemavu toka kijiji cha Ilemba alisema
ameweza kununua pikipiki kutokana na mkopo wa Milioni 2.5 hatua inayomwezesha
kupata kipato cha kuutunza familia na shughuli za kilimo.
Mnufaika huyo
aliwaambia wajumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa wa Rukwa kuwa kwa sasa anamiliki pia
bajaji kutokana na mkopo aliopata awali ambapo ametoa wito kwa halmashauri
kuwapa pia wahitaji wengine mikopo ikiwemo vijana kwa masharti nafuu.
“Ninaahidi nitajitahidi
kufanya marejesho ili walemavu wengine wapate mikopo hii. Sasa napambania uzee
wangu ili niwe na amani uzeeni kwa kuwa na uhakika wa kipato” alisema
Mwendapole.
0 Maoni