Na mwandishi wetu
Amesema Maalim Seif Sharif Hamadi alikua mwana maridhiano wa kweli na kielelezo halisi
ni juhudi zake katika kuhakikisha Nchi inakua na amani baada ya uchaguzi Mkuu wa
Mwaka 2020.
Dr Mwinyi amezitoa taarifa hizo hii leo
katika Maadhimisho ya Kumbukumbu ya Maisha ya Maalim Seif Sharif Hamad, katika
ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip, iliyopo Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid
Amani Karume Zanzibar, Mkoa wa Mjini Magharibi ambapo mgeni rasmi ya hafla hiyo
alikuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan.
“Mimi binafsi, nimebahatika kufanya kazi kwa
karibu sana na hayati Maalim Seif Sharif Hamad akiwa ni Makamu wangu wa Kwanza
wa Rais katika hii Awamu ya Nane ya Uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar chini ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa”.
“Bahati mbaya sana kutokana na kudra na uwezo
wa Mwenyezi Mungu hatukubahatika kuwa nae kwa kipindi kirefu sana ndani ya
uongozi wa Serikali hii na Mwenyezi Mungu kumpenda zaidi na kumchukua, hakika
pengo lake haliwezi kuzibika ndani ya Serikali na katika Jamii ya Wazanzibari
na Watanzania kwa ujumla”,alisema Rais Dk. Mwinyi.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi alisema
kuwa Maalim Seif hakuwa ni mtu mwenye kujikweza, kiburi au majivuno daima
alikuwa ni mtu alieweka maslahi ya Zanzibar kwanza na hakuwa mbinafsi wala
mchoyo katika kushauri au kutoa hekima na nasaha zake kwa viongozi vijana wao.
Aliongeza kuwa katika kipindi alichofanya
kazi nae aliweza kuvuna na kujifunza kwake mambo mengi yenye lengo la kufunza
na kuthamini mshikamano, maelewano na maendeleo ya nchi kwa jumla.




0 Maoni