Na mwandishi wetu
RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema katika
kipindi cha mwaka mmoja wa uongozi wake unaokuja serikali ina jumla ya shilingi
bilioni 460 ambazo zitaingizwa katika uchumi wa Zanzibar.
Dk. Hussein alitoa
kauli hiyo wakati akizungumza na wananchi moja moja na wananchi kupitia vyombo
vya habari katika ukumbi wa hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa ndege ikiwa ni
maadhimisho ya mwaka mmoja wa uongozi wake.
Alisema fedha
hizo ni pamoja na mkopo wa IMF wa dola za kimarekani milioni 100 sawa na
bilioni 230 ambazo ni mgao uliotoka katika serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa
Tanzania na mkopo uliokopwa na serikali ya Zanzibar wa shilingi bilioni
230.
Aidha alisema
lengo la kuingiza fedha hizo katika uchumi wa Zanzibar ni kuhakikisha kipindi
cha mwaka mmoja unaokuja ni kuona ahadi zote zilizoahidiwa kwa wananchi ziweze
kutekelezwa kwa ufanisi mkubwa kuliko mwaka mmoja uliotangulia.
Rais Mwinyi,
alisema hatakuwa na muhali kwa kiongozi yoyote atakaechukua theluthi ya fedha
hiyo kwa ajili ya maslahi yake binafsi.
“Bilioni 460 ni fedha
nyingi hivi tukikosa uadilifu fedha nyingi zitaingia kwenye mifuko ya watu
hivyo natoa idhari hata fedha moja isipotee sitasita kumfukuza mtu na kumpeleka
mahakaani,” alisema.
Dk. Mwinyi
akizungumzia fedha za IMF alisema fedha zake zitaingizwa katika sekta maalum
zilizoathirika na ugonjwa wa Uviko 19 ikiwemo sekta ya afya, elimu, maji, umeme
na kuwawezesha wajasiriamali.
Kwa upande wa
fedha za serikali za shilingi bilioni 230 zilizokopwa Rais Mwinyi alisema
zitaelekezwa katika maeneo matatu makubwa ikiwemo kulipa madeni ya wazabuni
wanaodai serikali, watu wanaostahili kulipwa fidia ambazo hawajalipwa na madeni
ya wafanyakazi wanaoidai wa serikali, barabara za ndani na kutoa fedha hizo kwa
ajili ya kuchangamsha uchumi kwa kuingiza fedha hizo katika mzunhuko ili
shughuli ziendelee kama ilivyokuwa kabla ya ugonjwa wa korona.
SEKTA YA AFYA
Dk. Mwinyi
alisema ili kuweza kuimarisha vyema sekta ya afya jumla ya shilingi bilioni 69
kwa ajili ya kuimarisha miradi ya miundombinu ya afya ikiwemo ujenzi wa
hospitali mpya ya ngazi ya Mkoa katika mkoa wa Mjini Magharibi katika eneo la
Lumumba ambao ujenzi wake utagharimu shilingi bilioni 14.
Alisema
hospitali hiyo itakuwa na uwezo wa kulaza wagonjwa 200 kwa wakati mmoja na
itakuwa ya horofa tano na kuwekwa vifaa tiba vya kisasa ikiwemo Seat Scan, IMR,
huduma za uchunguzi za maaba za kisasa na huduma za afya za dharura.
Dk. Mwinyi
alibainisha kwamba hospitali hiyo itakuwa na uwezo wa kutoa huduma mbalimbali
za kibingwa pamoja na huduma za macho na meno, wodi na kilnik za wagonjwa
mbalimbali kwa nia ya kuongeza wigo wa kutoa huduma bora na kupunguza idadi ya
watu wanaokwenda hospitali ya Mzanzimmoja ambayo nayo itaendelea kuboreshwa
kupitia msaada wa jumuiya ya Benki za kiarabu Badea ili ikidhi hadhi yake ya
kuwa hospitali ya rufaa.
Sambamba na
hilo, Rais Mwinyi, alisema serikali imeamua kutumia fedha hizo za IMF kuboresha
na kuipatia vifaa vya kisasa na madaktari wataalamu wa kutosha hospitali ya
Abdalla Mzee kisiwani Pemba na kuipandisha hadhi kuwa spitali ya mkoa ili iweze
kutoa huduma bora kwa wananchi wa mkoa wa kusini na kisiwa cha Pemba kwa
ujumla.
Hata hivyo
alisema pamoja na ujenzi huo serikali itajenga hospitali za wilaya 10 katika
ngazi ya wilaya ambayo kila moja itakuwa na uwezo wa kulaza wagonjwa 100 kwa
wakati mmoja pamoja na ujenzi wa nyumba za wafanyakazi zitakazotosha kuhudumia
familia 16 kwa gharama ya shilingi bilioni 22.
“Kwa mara ya kwanza
Zanzibar tutakuwa na hospitali mbili za mikoa hospitali 10 katika kila wilaya
zote za Unguja na Pemba isipokuwa wilaya ya Mkoani pekee na tayari michoro ya
hospitali zote imeshakamilika na taratibu za manunuzi ili kuwapata wakandarasi
zitatangazwa rasmi ambapo kazi ya ujenzi itaanza rasmi kabla ya mwezi wa
Disemba mwaka huu,” alisema.
Alisema
hospitali hizo zitatoa huduma za uchunguzi kwa kutumia vifaa vya kisasa Digital
XRAY Utrasoud, maabara za kisasa, ICU na wodi maalum kwa wagonjwa wanaohitaji
uangalizi wa karibu, magonjwa ya wanawake, upimaji wa mimba, uzazi wa kawaida
na huduma za upasuaji.
Alisema pia serikali
itanunua gari 12 za kubebea wagonjwa ambayo kila moja itawekwa katika hospitali
ya wilaya pamoja na hospitali mbili za mikoa huku gari tano kwa ajili ya
kusambazia dawa katika hospitali na vituo vya afya Unguja na Pemba kutoa bohari
ya dawa.
Dk. Mwinyi
alisema serikali itanunua mitambo ya kuchomea taka za hospitali kwa hospitali
zote za wilaya na Mikoa kati ya mitambo hiyo miwili itakuwa na uwezo mkubwa wa
kuchoma taka hatarishi ambayo itafungwa katika hospitali za mikoa ili iweze
kutoa huduma katika hospitali za karibu za serikali na binafsi.
Alibainisha
kwamba huduma za damu salama zitaimarishwa kwa kupatiwa vitendea kazi muhimu
zinavyoendana na mahitaji husika ili iweze kutoa huduma muda wote.
Hata hivyo
alibainisha kwamba serikali itanunua mitambo miwili katika hospitali za
Pangatupu na Abdalla Mzee za kuzalisha gesi tiba kila mmoja ukiwa na uwezo wa
kuzalisha mitungi 400 kwa siku itakayotumika kwenye hospitali nyengine Unguja
na Pemba zitakazohitaji huduma hiyo.
Alisema faida
zitakazopatikana baada ya kukamilika miradi hiyo ni kuona huduma bora za afya
karibu na wananchi na kutimiza dhamira ya kupunguza idadi ya wagonjwa
wanaosafirishwa nje ya Zanzibar kwa ajili ya kufuata matibabu.
Aidha alisema
utwekelezaji wa miradi hiyo mikubwa ya ujenzi wa miundombinu ya afya katika
wilaya zote za Unguja na Pemba ni utekelezaji wa dhamira ya serikali ya tangu
Mapinduzi yam waka 1964 ya kuwapatia huduma bora na sahihi za afya wananchi wa
Zanzibar.
SEKTA YA ELIMU
Kwa upande wa
sekta ya elimu Rais Mwinyi alisema serikali imetenga jumla ya bilioni 69 sawa
na dola za kimarekani milioni 30 ya fedha za mkopo wa IMF kwa ajili ya kufanyia
kazi changamoto mbalimbali zilizokuwepo katika sekta ya elimu na kuimarisha
kiwango cha elimu inayotolewa nchini.
Alisema serikali
itajenga madarasa 425 yaliyoanzishwa na nguvu za wananchi ambapo shughuli hiyo
itagharimu jumla ya shilingi 7.6 na ujenzi wamadarasa mapya 706 katika wilaya
zote Unguja na Pemba kwa ngazi ya maandalizi, msingi na sekondari.
Alisema madarasa
hayo yatajumuisha ujenzi wa madarasa mapya nay ale yatakayojengwa kuvutia
ujenzi wa skuli mpya 35 zikiwemo skuli 22 za Maandalizi, 13 msingi na sekondari
Unguja na Pemba ambapo skuli saba kati ya hizo zitakuwa za horofa.
Akitaja maeneo
yatakayojengwa skuli hizo alisema ni pamoja Mwanakwerekwe, Mtopepo, Bweleo na
Kwahani kwa Unguja na Mwambe, Kwale na Makangale kwa kisiwa cha Pemba na skuli
mbili katika eneo la Jendele kwa Unguja na Chake Chake kwa Pemba ambazo
zitakuwa maalum kwa ajili ya elimu mjumuisho.
Maeneo mengine
ya ujenzi wa skuli hizo alisema ni Mpendae, Kipapo, Pujini na Mgelema ambapo
ujenzi huo utagharimu jumla ya shilingi bilioni 43.9.
Vile vile
alibainisha kuwa serikali imeamua kuelekeza jumla ya shilingi bilioni 6.8 kwa
ajili ya ujenzi wa vyoo 1693 vya wanafunzi katika ngazi zote za elimu huku
jumla ya bilioni 7.8 zitatumiwa kwa ajili ya ukarabati wa skuli 22 ikiwemo
skuli ya Hailesalase, Chaani, Mlemani, Matemwe na Uzini kwa Unguja na Konde,
Chasasa na Kiwani Mauwani Pemba.
Katika sekta
hiyo pia alisema serikali itanunua vikalio 8000 kwa skuli ya ngazi ya msingi
zitakavyogharimu jumla ya shilingi bilioni 2 sambamba na ujenzi wa nyumba 10 za
walimu katika maeneo ya visiwa vidogo vidogo ikiwemo Tumbatu, Uzi, Njao, Kokota
na Ngambwa ambapo ujenzi wake utagharimu jumla ya shilingi milioni 600.
Alibainisha
kwamba serikali itatumia wakandarasi wakubwa wa daraja la kwanza, lapilli na
daraja la tatu kuhakikisha ujenzi huo unakuwa wenye ubora unaotakiwa kwani
taratibu za kuwapata wakandarasi hao zinaendelea ambapo serikali inatarajia
kusaini mikataba na kuanza kwa utekelezaji wa miradi kuanzia mwezi Disemba
mwaka huu.
Raid Mwinyi
alisema gharama zote za ujenzi pamoja na michoro ya majengo ya skuli mpya
imeshakamilika kwani serikali ina mafanikio makubwa ya utekelezaji wa miradi
yote hiyo ili kuweza kutoa elimu bora kwa watoto ambao ndio warithi wa
taifa.
Alisema ni imani
yake kwamba miradi hiyo ya ujenzi wa miundombinu ya elimu na afya itachochea
sana mzunguko wa fedha kwa kutoa ajira kwa makundi mbalimbali ikiwemo mafundi
uwashi, seremala, mama lishe na makundi mbalimbali sambamba na kukuza biashara
hasa vifaa vya ujenzi ikiwemo saruji, nondo na vifaa nyengine.
SEKTA YA MAJI
Alisema katika
kuzitapita ufumbuzi changamoto zilizokuwepo katika sekta hiyo alisema serikali
imetenga jumla ya shilingi 34.2 ambazo zitatumika kwa ajili ya kazi kuu tatu
ikiwemo kuongeza uzalishaji wa maji kwa kuchimba visima 28 Unguja na Pemba.
Aidha alisema
visima hivyo vinategemewa kuzalisha jumla ya lita za maji milioni 14.1 kwa siku
ambayo shunguli hiyo itatumia shilingi bilioni 2.1 na ununuzi wa vifaa
mbalimbali ambavyo vitasaidia katika uchimbaji wa visima ambapo imepanga kutumia
jumla ya shilingi bilioni 2.1 huku itatumia shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya
kuviendeleza visima 36 Unguja na Pemba vilivyochimbwa kupitia mradi wa Ras
alhema ambavyo vinatengemewa kuzalisha lita za maji 15.7 milioni kwa siku.
Sambamba na hatua
hizo alisema pia watafanya ukarabati visima vilivyowekewa pampu chini ya
kiwango ambapo jumla ya visima 49 Unguja na Pemba zinategemewa kubadilishwa
mashine na kutiwa mashine zenye uwezo unaostahiki kwa mujibu wa uwezo wa visima
hivyo ambavyo vinategemewa kuzalisha lita za maji 23.4 milion kwa siku ambapo
jumla ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya kazi hiyo ni shilingi bilioni 6.9.
Alisema kupitia
fedha hizo serikali imepanga kubadilisha bomba za maji chakavu na kusambaza
bomba mpya kwa maeneo ambayo huduma ya maji haijafika ambapo jumla ya kilomita
319 zinategemewa kubadilishwa na kuboreshwa mtandao wa maji ambapo bilioni 8.2
zimepangwa kwa ajili ya kazi hiyo.
Kadhalika
alisema serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 210 kwa ajili ya kukarabati
matangi ya maji Unguja na Pemba kwa lengo la kuongeza kiwango cha uhifadhi wa
maji ambapo kwa Unguja matangi mawili na Pemba tangi moja yote yakiwa na uwezo
wa kuhifadhi lita milioni 3.2.
Alisema pia
serikali imetenga shilingi bilioni 12 kwa ajili ya ujenzi wa matangi mapya tisa
yenye ujazo wa lita milioni 1 kila moja Unguja matangi matano na Pemba matangi
manne ambapo jumla ya lita za maji milioni 9.2 zinatarajiwa kuhifadhiwa katika
matangi hayo.
“Kwa kipindi kifupi
kijacho tumedhamiria kuongeza kiwango cha maji kutoka lita milioni 131 kwa siku
sawa na asilimia 55 hadi lita 170 milioni sawa na asilimia 71 ya mahitaji ya
siku kwa wananchi,” alibainisha.
Dk. Mwinyi
alisema serikali itaiwezesha Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kwa kununua magari
mawili ya kuchimba visima kwa Unguja na Pemba.
SEKTA YA NISHATI
Kwa upande wa
sekta ya umeme alisema serikali imetenga shilingi bilioni 11 kati ya fedha za
mkopo wa IMF kwa lengo la kuzitafutia changamoto zilizojitokeza katika sekta
hiyo ambapo fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kupunguza gharama za watu
wanaotaka kuvuta umeme wananchi wa Unguja na Pemba ambapo wastani wa wateja
30,000 wanatarajiwa kufikiwa.
Alisema hatua
hiyo itajumuisha ujenzi wa miundombinu ya umeme mkubwa pamoja na ununuzi wa
vifaa mbalimbali zitakavyotumika katika kazi hiyo ambapo katika mpango huo
muombaji wa umeme atachangia shilingi 200,000 badala ya shilingi 600,000 na
gharama zilizobaki zitafidiwa na serikali.
Alifahamisha
kuwa lengo la uamuzi huo wa serikali kupunguza gharama za uungaji wa umeme kwa
wananchi ni kuwapunguzia gharama hizo ili kuweza kumudu huduma hiyo kwa maisha
ya kila siku.
SEKTA YA UWEZESHAJI
WANANCHI KIUCHUMI
Alisema katika
kipindi cha kampeni alikutana na makundi mbalimbali kwa ajili ya kujadili
maendeleo na kufahamu changamoto zinazowakabili ikiwemo makundi ya vijana,
waendesha bodaboda, mama mtilie, wavuvi, wachonga mbao, wafanyabiashara
masokoni na makundi mengine.
Rais Mwinyi alisema
katika kutatua changamoto ya makundi hayo hasa kukosekana kwa mitaji serikali
imetenga shilingi bilioni 85.4 kwa shughuli za uwekezaji wananchi kiuchumi kwa
ajili ya kuwaendeleza wajasiriamali hao Unguja na Pemba katika sekta ya uchumi
wa bluu na sekta nyengine za uwezeshaji.
Alisema serikali
ya awamu ya nane imedhamiria kuleta mageuzi ya kiuchumi kwa kutekeleza sera za
mipango na kuendeleza uchumi kwa ujumla kwani aliahidi na amedhamiria
kutekeleza ahadi alizozitoa kwa wananchi wa Zanzibar.
Alifahamisha
kuwa katika fedha hizo za mkopo amelekeza jumla ya shilingi bilioni 36.5 kwa
ajili ya kuwawezesha wajasiriamali wa sekta ya uvuvi na mazao ya baharini.
Alisema kati ya
fedha hizo bilioni 20 zitatumika kwa ajili ya kuwapatia vikundi vya wavuvi boti
577 za kisasa zenye vifaa muhimu vya uvuvi ikiwemo mitengo ya kisasa ya kuvulia
na majokofu ya barafu ambapo mpango huo utawanufaisha wavuvi wasiopungua 5,770.
Rais Mwinyi
alisema juhudi kubwa zitaelekezwa katika kuwapatia wananchi na wajasiriamali
31,770 vifaa vya uvuvi na ufugaji wa mazao ya baharini pamoja na usarifu wa
dagaa.
Alisema serikali
imetenga bilioni 2.5 kwa ajili ya kuwaendeleza wakulima wa mwani ambapo jumla
ya vihori 500 vitanunuliwa hivyo matumaini yake kwamba jumla ya wakulima wa
mwani 5,000 watanufaika na mpango huo.
Alibainisha kuwa
shilingi bilioni 1.7 zitatumika kwa aili ya ununuzi wa vifaa kwa ajili ya
kuendeleza za hilo na ukamilishaji wa kiwanda cha mwani kisiwani Pemba kwa
thamani ya shilingi milioni 500 kwa lengo la kusaidia uogezaji wa thamani ya
zao la mwani ili kuongeza tija ya zao hilo.
Mbali na hayo,
alisema serikali imetenga shilingi bilioni 1.1 kwa ajili ya kuviwezesha vikundi
100 vya ufugaji wa majongoo ya bahari Unguja na Pemba na jumla ya shilingi
milioni 402 zitatumika katika kuendeleza vikubndi 60 vya ufugaji wa kaa na
bilioni 1.2 zitatumika kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali
wanaojishughulisha na ufugaji ambapo jumla ya vikundi 40 vitanufaika na mpango
huo.
Rais Mwinyi
alisema fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya kuendeleza uchumi wa bluu ni
kuhakikisha zinawanufaisha wananchi 1,580,850 katika myororo mzima wa thamani
ambayo ni hatua muhimu katika kutekeleza ahadi ya kukuza ajira nchini.
Kwa upande wa
sekta nyengine za kiuchumi serikali imetega jumla ya shilingi 5.6 kwa ajili ya uwekezaji
wajasiriamali wa sekta nyengine ambapo unatarajia kuwanufaisha watu hao na
wafanyabiashara wadogo wapatao 101,704 kwa Unguja na Pemba.
Alisema jumla ya
shilingi bilioni 4 zitatumika kwa ajili ya kunufaisha wafanyabiashara wenye
viwanda vidogo vidogo na vyakati katika sekta ya useremala, ushoni,
utengenezaji wa sabuni, usindikaji wa mazao, viwanda vya kusaga nafaka na
viwanda nyengine.
Hata hivyo
alisema jumuiya za waendesha bodaboda kila mkoa watakopeshwa kwa kuanzia
bodaboda 50 kwa ajili ya vijana wa mkoa husika hivyo jumla ya wajasiriamali
2,906 waliokuwa katika makundi hayo watanufaika katika mpango huo.
SEKTA YA KILIMO NA
UFUGAJI
Rais Mwinyi
alisema ni miongoni mwa sekta iliyopewa kipaumbele ambapo litakuwa na miradi
413 ambapo shilingi bilioni 6.7 zitatolewa ambazo zitanufaisha wakulima na
wafugaji 8,444.
Kwa wananchi
wanaojishughulisha na kazi za mikono ikiwemo wahunzi, watu wenye ulemavu,
wachoraji wa hina, watengenezaji wa mabango, mafundi gereji, wafinyanzi alisema
wametengewa jumla ya shilingi bilioni 5 ambazo zitawanufaisha wananchi wapatao
22,600.
Wafanyabiashara
wa maduka ya rejareja na jumuia masokoni, alisema makundi hayo yametengewa
shilingi bilioni 5.2 zitakazowanufaisha watu 950 Unguja na Pemba huku bilioni
2.5 kwa ajili ya mama lishe, baba lishe, wamiliki wa mikahawa vijana na
watengenezaji simu na vifaa vya umeme kama vile mafriji na kompyuta Unguja na Pemba
ambapo idadi ya wanufaika ni elfu 16.
Alisema sehemu
ya fedha hizo pia zitatumika katika ujenzi wa kituo cha kulea na kukuza
wajasiriamali ikiwemo kuwapatia mafunzo ya ufugaji wa nyuki ambapo jumla ya
wajasiriamali 5,834 ambapo pia katika fedha hizo serikali itaandaa maeneo
maalum ya kufanyia biashara kwa wajasiriamali wanaojishughulisha na biashara ya
welding, uhunzi na mbao na uchogaji wa thamani ili kuwawekea mazingira mazuri
ya biashara.
Rais Mwinyi
alisema hatokata taamaa wala kuvunjika moyo kwa watu wanaomkejeli katika
dhamira yake ya uchumi wa bluu kwani wapo wanaofanya kejeli katika dhana hiyo.
“Nimedhamiria
kwani niliyoyasema yote yapo ndani ya dhamira yangu na wahenga wanasema nia
njema hairogwi mwaka wa kwanza ulikuwa ukidorora lakini fedha hizi zitaingia
katika mzunguko wa uchumi,” alibainisha.
Aliwahakikishia
wananchi wa Zanzibar kuwa fedha hizo zikiingia basi kila mtu atanufaika kwani
fedha hizo zitagusa sekta zote hivyo mwaka wa piliwa serikali ya awamu ya nane
utakuwa wa mafanikio zaidi.
Kwa upande wa fedha za
mkopo zilizokopwa na serikali bilioni 230 alisema zitatumika kwa ajili ya
kuongeza mzunguko wa fedha na wafanyabiashara kwa wananchi ikiwemo ulipaji wa
madeni makubwa ambayo serikali inadaiwa nawazabuni, wastaafu, wananchi na wafayakazi
wa serikali.
Alisema
serikali imefanya maamuzi kuwalipa wananchi waliowekeza fedha zao katika
kampuni ya master life ili kuwasaidia wahanga hao ambao wameathirika na
matapeli ambapo shilingi bilioni 6.7 zimepatikana katika akaunti yao.
Aliwasisitiza
wananchi kuendelezxa amani ya nchi yao kwani tayari ndani ya jamii yapo maneno
yameanza kuashiria uvujifu wa amani yanayotolewa na baadhi ya viongozi ambao
wanataka kuichafua amani iliyopo nchini.
Hata hivyo
aliwasisitiza viongozi kuanzia ngazi ya shehia kuhakikisha wanawajibika katika
utekelezaji wa majukumu yao katika kuwatumikia wananchi wa Zanzibar.
Akiongea kwa
njia ya simu Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan,
alimpongeza Dk. Mwinyi kwa kutimiza mwaka mmoja wa uongozi wake na kuwataka
wazanzibari kushikana kwa pamoja katika kuendeleza umoja amani na mshikamano
kwa lengo la kuijenga Zanzibar yao.
Alisema huu ni
mwaka mmoja wa uongozi wa Rais Mwinyi hivyo ni vyema wananchi wakaendelea
kushikamana ili kuifikisha Zanzibar kiuchumi na kimaendeleo.
Mwenyekiti wa
kamati ya sherehe ya kutimiza mwaka mmoja wa uongozi wa Dk. Hussein Ali Mwinyi
Iddrissa Kitwana Mustafa, alisema katika maadhimisho hayo yamefanyika mambo
makubwa ikiwemo uzinduzi wa miradi mikubwa na yenye kuleta tija kwa wananchi wa
zanzibar.
Alisema miradi
hiyo ilipata nafasi ya kuwekewa mawe ya msingi imeonesha ari ya maendeleo ya
serikali ya awamu ya nane kutokana na kasi ya ujezi wake ndani ya kipindi cha
mwaka mmoja tu.
0 Maoni