MHE: Rashid Hadid Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja 


 Na mwandishi wetu

Halmashauri ya Wilaya ya Kusini imefanikiwa kukusanya kiasi cha Shilingi Milion Sabiin na Saba na Tisini na Nane Mia Saba na Nane (Tsh 7,798,708) kwa kipindi cha Miezi Mitatu ya Robo ya kwanza kuanzia Julai hadi Sept mwaka huu.

 Akiwasilisha ripoti ya utekelezaji ya kamati ya Fedha, Mipango na Uchumi, katika kikao cha Baraza la Madiwani lililofanyika leo katika Ukumbi wa Halmashauri hiyo Kitogani Kusini Unguja,  mjumbe wa Kamati hiyo Sharifa Omar Ali, amesema Halmashauri ya Kusini awali ilipanga kukusanya Jumla ya Shilingi Milion  Sabiini na Sita lakini imefanikiwa kukusanya Milion Sabiin na Saba sawa na Asilimia Mia na Moja hali ilopelekea kuvuka malengo waliojipangia.

 Amesema hatua hio imefikiwa kutokana na kuongezeka kwa vyanzo vipya vya mapato ikiwemo usafirishaji wa Mali Asili, Leseni za Vileo na Maduka, Nyumba za kulaza wageni, minara pamoja na malipo ya faini za uchafuzi wa mazingira na kuchelewa kukata Leseni.

 Mapema Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Ndugu  Ali Rashid Suluhu amesema mbali na mafanikio yaliopatikana katika ukusanyaji wa mapato lakini pia  amewasisitiza makatibu wa kamati ya kudumu za baraza hilo kuhakikisha wanafikisha kwa wakati taarifa za kamati zao wanazo ziandaa ili kuiwezesha halmashauri kufanya kazi zake kwa ufanisi.

 Nae Mwenyekiti wa Baraza la Halmashauri ya Wilaya ya Kusini ndugu Mustafa Mohd Haji amewataka watendaji wa halmashauri hiyo kuendelea kutimiza wajibu wao hasa katika suala zima la kuongeza vyanzo vya ukusaji wa mapato kwa lengo la kuleta maendeleo kwa Jamii na Serikali kwa ujumla.

 Kikao hicho cha baraza la Halmashauri kilichohudhuriwa na watendaji wa Chama na Serikali mbali ya kupokea ripoti mbali mbali za utekelezaji wa utendaji kazi wa Baraza hilo pia imeridhia na kupitisha vifungu vya matumizi ya Fedha  Shilingi Milion Mia Moja na Sitini na Saba zilizotumika kwa shughuli za Mishahara pamoja na ununuzi wa vifaa vya matumizi ya ofisi.