SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema inaendelea kufanya mazunguzo na taasisi za kifedha kwa ajili ya kuwapatia mikopo Pamoja na elimu ya ujasiriamali wanawake wajane waliofiwa ama kuachwa na waume zao na kuachiwa mzigo wa ulezi wa familia ili kuwasaidia kukabiliana na hali ya umaskini wa kipato..

 Akitoa ufafanuzi baada ya kupokea malalamiko kutoka kundi la wanawake wajane, katika Viwanja vya Kinyasini Kisiwani Pemba , Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe Dkt Hossein Ali Mwinyi amesema njia ya pekee ya kuwasaidia ni kuwapatia elimu ya ujasiriamali Pamoja na kuwatafutia soko la kuuzia bidhaa zao.

 Amesema  Serikali inatambua na kuthamini kazi wanazofanya, lakini kunahitajika kupatiwa elimu ya ujasiriamali ili bidhaa wanazozalisha ziweze kuuzika katika masoko ya ndani na nje

 Mapema wanachama wa Jumuiya ya wajane Zanzibar kanda ya Pemba wamesema bado hawajanufaika na misaada inayotolewa na Serikali na kuiomba Serikali kuongeza nguvu katika kulisaidia kundi hilo.