Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akisalimiana na Wananchi wa Kijiji cha Zinga Bagamoyo alipokuwa njiani akielekea Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani leo Sept 02,2021 kwa kwa ajili ya kuendelea kurekodi kipindi maarufu cha Royal Tour kitakachotangaza Utalii, Biashara na Uwekezaji Nchini. 
Na mwandishi wetu

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, amesema pamoja kuwa tozo za miamala ya simu zimepunguzwa kwa asilimia 30 lakini tozo hizo ni muhimu kwa kuwa zinachangia upatikanaji wa huduma muhimu za jamii

Mhe. Rais Samia amesema hayo leo tarehe 02 Septemba, 2021 wakati aliposimama kuwasalimia wananchi wa Tegeta  Jijini Dar es Salaam na Zinga, Bagamoyo mkoani Pwani wakati akielekea Bagamoyo mjini kuendelea kurekodi vivutio mbalimbali vya utalii katika kipindi   maarufu cha Royal Tour.

Amesema Serikali imeamua kuweka tozo hiyo kwa dhamira ya kuleta mabadiliko katika sekta mbalimbali za huduma ambapo katika kipindi cha miezi miwili Serikali kupitia tozo hizo imejenga vituo vya afya 220 pamoja na ukamilishaji wa madarasa 560 katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, Mhe. Rais Samia amewahakikishia wananchi hao wa Tegeta (Dar es Salaam) na Zinga (Bagamoyo) kuwa miradi yote ya kimkakati iliyoanzishwa na Serikali ya Awamu ya Tano inakamilika kama ilivyokusudiwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi CCM pamoja na miradi mingine mipya.

Akizungumzia ujenzi wa mradi wa Bandari ya Bagamoyo, Mhe. Rais Samia amesema mradi huo ni mkubwa na Serikali kwa sasa inaupitia upya ili ijiridhishe kwasababu utasaidia kutoa ajira na kukuza uchumi wa pamoja na kuboresha huduma za kijamii.

Kuhusu UVIKO 19, Mhe. Rais Samia amewataka wananchi kuona umuhimu wa kupata chanjo kwani ugonjwa huo bado upo na unaendelea kupoteza maisha kwa wananchi.

 Mhe. Rais amewataka viongozi wa mkoa wa Pwani kuhakikisha wanamaliza migogoro ya wakulima na wafugaji katika mkoa huo ili wananchi wawendelee na shughuli za maendeleo kwa amani na utulivu.

Mapema Mbunge wa Jimbo la Kawe Mhe. Askofu Josphat Gwajima, Mhe. Ridhiwani Kikwete Mbunge wa Chalinze na Mhe. Muharami Mkenge Mbunge wa Bagamoyo wamempongeza Mhe. Rais Samia kwa jitihada mbalimbali anazofanya katika kuwaletea maendeleo wananchi na kuahidi kuendelea kushirikiana naye.