Uongozi wa Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Uchukuzi umetakiwa kuweka utaratibu mzuri wa kuwahudumia wananchi wanaofika kupata huduma katika Idara ya Usafiri na Leseni.
Makamu wa Pili wa Rais
wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ameeleza hayo wakati alipofanya ziara
ya kushtukiza katika Mamlaka ya Usafiri na Usalama Barabarani iliyopo
Mwanakwerekwe Wilaya ya Magharibi ‘’B’’ Unguja.
Amesema Serikali
inahitaji mapato katika uendeshaji wa kazi zake hivyo mamlaka hiyo ina jukumu
la msingi la kuweka utaratibu imara utakaosaidia kuingizia serikali mapato, ili
kusaidia kukuza uchumi wa Nchi.
Akizungumzia juu ya
suala la kughushi nyaraka feki Mhe. Hemed alimuagiza Mkurugenzi Mkuu Mamlaka
Usafiri na Usalama barabarani kuchukua hatua kali dhidi ya watu watakaobainika
kufanya vitendo hivyo ikiwemo kuwafikisha mahakamani ili wachukuliwe hatua za
kisheria.
Katika hatua nyengine
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo
kuangalia namna bora ya kuimarisha ulinzi katika eneo la maegesho ya magari kwa
kufunga Kamera za usalama ili kudhibiti uhalifu unaojitokeza mara kwa mara.
Aidha, aliwataka
wananchi wanaofika kupata huduma katika mamlaka hiyo kujenga tabia ya uaminifu
na kauchana na vitendo vya utapeli ikiwemo kughushi nyaraka za Serikali ili
kujenga mashirikiano mazuri na wafanyakazi wa idara hiyo.
Akijibu baadhi ya
changamoto zilozotolewa na wananchi Mkurugenzi Mkuu mamlaka ya Usafiri na
Usalama barabarani Haji Ali Zubeir alisema mamlaka anayoisimamia imekuwa
ikichukua hatua kwa wananchi wanaokiuka taratibu ili kuondosha vitendo vya
kihalifu ikiwemo kughushi nyaraka feki za Leseni.
Ameeleza kuwa, mamlaka
ya Usafiri na Usalama barabarani imekuwa ikisimamia sheria kwa wanafunzi
wanaojifunza udereva kwa kutumia gari za manual badala ya automatic ili
kuwajengea umahiri wanafunzi hao na kupunguza idadi ya ajali na athari mbali
mbali wanapokuwa Barabarani.





0 Maoni