Makamu wa Kwanza wa rais wa Zanzibar Mhe. Othman Msoud Oudhman, amesema Zanzibar na Oman zinaweza kutumia historia na uhusiano wa damu uliopo wa muda ili kuibua fursa mpya zaidi za uwekezaji ili  kusaidia kukuza uchumi na maendeleo ya kijamii.

Mhe. Othman ameyasema hayo leo Ofisini kwake Migombani mjini Zanzibar, alipozungunza na Balozi Mdogo wa Oman aliyepo Zanzibar Mhe. Said Salim Al Sinawi.

Aidha amefafanua kwamba yapo maeneo mengi ambayo kimsingi, yanaweza kujadiliwa zaidi na baadae kujengewa ushirikiano unaoweza kusaidia manufaa kwa Zanzibar na Oman.

Mhe Othman amemueleza Balozi Al Sinawi kwamba Suala la mahkama ya Kadhi, fursa za masomo na kubadilishana uzoefu ni miongoni mwa maeneo muhimu, ambayo serikali hizo mbili zinaweza kujadiliana na kukubaliana kuongezwa ushirikiano kwa kuwa yana mchango mkubwa katika historia Oman na Zanzibar.

Amesema kwamba Oman inazoefu mkubwa katika kusimamia mahkama za kadhi na kwa vile ni waazilishi wa mahakama hiyo hapa Zanzibar ni muhimu kuongeza ushirikiano katika kusaidia mbinu za uendeshaji na usimamizi wa hakama hizo  Zanzibar.

Pia Mhe. Othman alimweleza Balozi huyo kwamba hivi sasa Zanzibar inatekeleza sera yake ya Uchumi wa Bluu, na imeweka  mazingira mazuri ya uwekezaji ambayo yanaweza kutumika kama fursa ya kuendeleza uwekezaji na kusaidia nchi kukuza uchumi.

Naye Balozi Al Sinawi alimueleza Mhe. Makamu kwamba , Oman ipo tayari kuendeleza ushirikiano wa historia uliopo katika sekta mbali mbali na kwamba anaichukulia Zanzibar kuwa ni nyumbani kutokana udugu wa damu uliopo kwa muda mrefu.

Aidha amesema kwamba serikali ya Oman ina nia thabiti ya kusaidia Zanzibar na Tanzania kwa jumla katika maeneo mabali mbali, licha kwamba maradhi ya UVIKO 19 imekuwa ni kikwazo kikubwa katika utekelezaji wa mambo mbali mbali hivi sasa.

Pia Mhe. Sinawi amesema kwamba nchi yake na Zanzibar tayari inayomakubaliano ya ushirikiano katika kuendeleza sekta ya biashara  utalii ambayo inasaidia sana kukuza uchumi na maeneleo.