Waziri wa nchi, ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Idara maalum za SMZ, Masoud Ali amewataka watoaji huduma za wakala za kijamii kuacha urasimu katika utoaji wa huduma hizo.

Amewasisitiza watendaji wa taasisi hiyo hususani wale wa chini kutekeleza vyema majukumu yao vyema, kuwa na majibu mazuri pamoja na kutoa huduma kwa wakati ili kupunguza msongamano wa wananchi katika ofisi hiyo.

Aidha amewataka watendaji wa ofisi hiyo ya wakala wa huduma za Kijamii iliyopo Mazizini, Unguja kuzingatia sheria namba 3 ya mwaka 2018 ya matukio ya kijamii kutambua mfumo na vigezio vya utoaji wa huduma ya upatikanaji wa vyeti vya kuzaliwa ili kuondoa changamoto ya utoaji wa vyeti hivyo kwa wale wasio na uhalali.

Sambamba na hayo licha ya kuahidi kutetea maslahi ya watumishi wa taasisi hiyo amewataka kuacha tabia ya kushirikiana na vishoka katika utoaji wa vyeti feki kwani hatua hiyo inachochea ongezeko la vyeti feki.

Ameonya kuwa Serikali itachukua hatua kali kwa mtumishi yeyote atakaebainika kujihusisha na vitendo hivyo.