Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Selemani Jafo (mbele) akiwa na Meneja wa Kanda ya mashariki  kaskazini Bw. Anorld Mapinduzi wakati wa ukaguzi wa mazingira kwenye kiwanda cha Sayona kinachomilikiwa na Kampuni ya Motison Group.

 Na mwandishi wetu

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Selemani Jafo ametoa miezi sita kwa wamiliki wa kiwanda Cha Sayona kinachomilikiwa na Kampuni ya Motison Group ambacho kinazalisha bidhaa za plastiki, rangi na Chuma kuhakikisha kinatenga eneo maalumu la kuhifadhia bidhaa za vinywaji ili kuepuka kuchanganyika na bidhaa  zisizo za chakula zinazo zalishwa kiwandani hapo.

Waziri Jafo ameyasema katika  ziara yake kwenye kampuni ya Motison Group inayomilikiwa na  kampuni ya Sayona, Mikocheni Jijini Dar es Salaam.

"Kiwanda hiki mmejitahidi kwenye mfumo wa kutibu maji, lakini tatizo nililolibaini ni kwamba mnaweka bidhaa za vinywaji sehemu moja na bidhaa  nyingine kama rangi na plastiki jambo ambalo ni hatari kwa afya zetu. Ninatoa miezi sita kuanzia sasa mtenge sehemu maalumu ya kuhifadhia bidhaa za vinywaji ili kuepuka madhara ya kiafya ya mtumiaji wa vinywaji mnavyozalisha hapa."

Katika hatua nyingine Waziri Jafo amekataa kusaini kibali cha kukusanya chuma chakavu kwenye kiwanda cha Iron & Steel kilichopo Mikocheni Jijini Dar es salaam mpaka kitakapoweka mfumo mzuri wa kuzuia moshi usisambae angani.

Waziri Jafo amechukua hatua hiyo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wakazi walio karibu na kiwanda hicho kutoa moshi unaoleta athari kwa afya zao.

" Viwanda vinatoa ajira kwa Wananchi wetu, mbali na hilo vinalipa kodi kwa Serikali yetu. Pamoja na hizi faida ni lazima tuzingatie utunzaji wa mazingira yetu. Kiwanda hiki hakina mfumo mzuri wa kutoa moshi jambo ambalo ni hatari kwa afya ya wakazi wa eneo hili, hivyo naagiza wafanye marekebisho ili wapate kibali cha ukusanyaji wa vyuma chakavu." amesema  Waziri Jafo.

 Aidha Waziri Jafo amekipongeza kiwanda cha Coca-cola kwanza kilichopo Mikocheni Jijini Dar es Salaam kwa jitihada na harakati za utunzaji wa Mazingira. Amewapongeza kwa kuunda mabalozi wa Coca-cola wanaokusanya chupa za plastiki kwa ajili ya kurejelezwa (recycling).