Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amesema vitendo vya ukeketaji vinaendelea nchini kwakuwa wnaume hawajaamua kuukataa.

Akizungumza Wilayani Tarime Mkoa wa Mara alipotembelea kituo Nyumba Salama cha Masanga kinachotumika kuwalea watoto waliokumbwa na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia au walio katika hatari ya kukumbwa na vitendo hivyo.

Dkt. Gwajima amesema ukeketaji unaweza kukomeshwa nchini endapo wanaume watakaa katika makundi yao na kujadiliana jinsi ya kukomesha vitendo hivyo.

Hata hivyo amesema wakati umefika kwa jamii kuachana na visingizio vinavyosababisha kuendelea kwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto na badala yake kusimamia misingi ya upatikanaji wa haki.

Awali Meneja wa Mradi wa kupinga Ukeketaji Kituoni hapo, Valerian Mgani amesema kituo hicho kinakabiliwa na changamoto ya bweni, chombo cha usafiri na watoto wa kike kukatishwa masomo, kukeketwa na ndoa katika umri mdogo.

Kituo cha Nyumba salama cha Masanga kilianzishwa mwaka 2006 na kusajili mwaka 2015 kwa lengo la kuwahudumia watoto wahanga wa ukatili ukiwemo ukeketaji ambapo hadi sasa kituo hicho kinahudumia walengwa 34 kati yao mmoja ni wa kiume.