Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew akikagua sifa (specifications) na ubora wa moja ya kompyuta 19 zilizonunuliwa katika Telesenta ya Sengerema kwa ufadhili wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) Richard

Na mwandishi wetu

Watumishi watatu wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema wanaosimamia Redio Sengerema 98.8 FM wanashikiliwa na jeshi la Polisi kwa ubadhirifu wa shilingi Milioni Ishirini na Saba laki Saba na Elfu Ishirini  (27,720,000).

Fedha hizo zilizopotea ni bakaa ya shilingi Milioni 103 zilizotolewa na taasisi ya mawasiliano ya Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kwa ajili ya kuboresha Telesenta ya Sengerema

Maamuzi hayo yametolewa na Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew baada ya kufika katika Telesenta hiyo na kusomewa taarifa ya matumizi ya fedha hizo iliyoonesha kuna bakaa ya shilingi Milioni 27,720,000 huku taarifa ya kibenki ya akaunti ya kituo hicho ikionesha fedha zote zimetumika na hakuna bakaa yeyote

Aidha, baada ya Mhandisi Kundo kuhoji kwanini taarifa ya kibenki inakinzana na taarifa waliyomsomea ndipo Meneja wa Kituo hicho Sostenes Tangalo kukiri kuwa wakati kituo kinapatiwa fedha na UCSAF suala la kurekebisha studio ya redio halikuwepo lakini katika manunuzi hayo ambayo yalifanyika kwa malipo ya fedha taslimu yaani cash wao wakaona wanunue na vifaa vya kurekebisha studio hiyo pamoja na samani

Baada ya maelezo hayo kuonesha kuna harufu ya ubadhirifu wa fedha za Serikali zilizotolewa na taasisi ya UCSAF ambayo ipo chini ya Wizara hiyo Mhandisi Kundo ameagiza Meneja wa Kituo hicho Sostenes Tangalo, mwanasheria Ilambona Mahuba na Afisa Habari kuwekwa ndani na taratibu za kisheria zifuatwe.

Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew akipitia taarifa ya manunuzi ya vifaa vya kituo Telesenta ya Sengerema. Kulia ni Mkuu wa Uendeshaji wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote Mhandisi Albert Richard