SERIKALI ya Mapinduzi
Zanzibar, imesema jumla ya watu 390 wamegundulika kuwa na maambukizi ya Virusi
vya korona hapa Zanzibar wakiwemo watanzania 112 na wageni 278 ambao walitoka
katika mataifa mbali mbali duniani.
Waziri wa Afya,
Ustawi wa Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto, Nassor Ahmed Mazrui, alitoa kauli
hiyo wakati akitoa tamko la Serikali kuhusu kuwepo kwa wagonjwa wa korona hapa
Zanzibar ambao unasambaa kwa kasi kubwa Ofisini kwake Mnazimmoja.
Alisema wagonjwa
hao ni kati ya watu 29,326 waliopimwa Virusi vya Corona (COVID-19) katika vituo
na Hospitali mbalimbali Unguja na Pemba kuanzia Juni 25 hadi Agosti 10 mwaka
huu .
Alisema kati ya
wagonjwa hao 390 waliothibitika, watu 207 wamepona na wagonjwa waliobaki 183
wakiwemo watanzania 32 na wageni 151 huku wagonjwa 24 wamelazwa na wanaendelea
na matibabu katika Hospitali mbali mbali hapa Zanzibar.
Waziri huyo
alibainisha kuwa kuanzia mwezi Juni hadi August, 2021 jumla ya vifo 15 vya
wazanzibari vilitokea vilisababishwa na ugonjwa wa homa kali ya mapafu
inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19) na kuripotiwa katika hospitali
mbalimbali hapa nchini.
Alibainisha kuwa
Zanzibar inakabiliwa na ugonjwa huo huku serikali imekuwa ikichukua hatua
mbalimbali za kudhibiti kuenea kwa ugonjwa huo hapa Zanzibar.
Akizungumzia
chanjo ya Korona amesema wizara inaendelea na hatua mbali mbali za kinga dhidi
ya ugonjwa huo ikiwemo utoaji wa chanjo.
Waziri huyo amesema
kwa sasa wameanza kutoa chanjo ya korona kwa makundi maalumu ambayo ni
hatarishi zaidi kuambukizwa ugonjwa huo.
Akiyata makundi
hayo alisema ni pamoja na wafanyakazi wa milango mikuu ya kuingia nchini
ikiwemo viwanja vya ndege na bandarini, wadau wa utalii wakiwemo waongoza
watalii, madereva wanaosafirisha wageni na watalii, wafanyakazi wa vyombo vya
usafiri vya ndani na nje ya nchi, wafanyakazi wa mahoteli, wazee kuanzia miaka
55 na watu wenye magonjwa sugu na ya muda mrefu.
0 Maoni