Madiwani
wa halmashauri ya Kishapu Mkoani Shinyanga wameiomba Serikali kuboresha miundombinu
ya barabara katika maeneo yao ili kuwaondolea wananchi adha ya kulazimika kutumia
mikokoteni ya Ng’ombe kusafirishia
wagonjwa hasa kipindi cha masika kutokana
na uchakavu wa miundombinu ya Barabara.
Hayo
wameyasema agost 27, 2021 kwenye kikao
cha baraza la madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa halmashauri hiyo, ambapo
wamesema hali ya barabara inayotoka Migunga, Mwataga kwenda Isoso wakati wa
masika hazipitiki hivyo huwaweka hatarini wananchi ambao ni wagonjwa kwa
kubebwa katika magaria ya Ng’ombe kwaajili ya kupelekwa Hospital.
Diwani
wa Kata ya Mwataga halmashauri ya Kishapu Mhe Matungwa Daudi na diwani wa Kiloleli
wamesema hali hiyo inapelekea wagonjwa wengine kupoteza maisha wakiwa wapo
njiani kutokana na kukosekana kwa miundombinu ya uhakika ya barabara na usafiri
'Tunaiomba serikali itusaidie juu ya hili
kutokana na barabara kuwa mbovu hazipitiki mwaka juzi kuna mama mmoja alipoteza
maisha kutokana na kukosekana kwa barabara, hivyo tunaomba barabara
zitengenezwe ili kunusuru afya za wananchi,amesema Daudi.
Kwa upande
wake Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo amesema kero za barabara zinaonekana
zipo kila kata hivyo Tarura iliangalie vizuri suala hili kwani wananchi
wanahitaji barabara waweze kupata matibabu kwa muda na waweze kusafirisha mazao
yao kwa wakati.
Kwa
upande wake Meneja wa Tarura Wilaya ya Kishapu Samson Pamphili amesema serikali
ilikuwa imetenga Sh 800.9 milioni lakini
baada ya kuona changamoto za barabara ni nyingi iliongeza fedha ikafika Sh 2.4
Bilioni ambazo zimeelekezwa kuishirikisha halmashauri na mbunge, na fedha hizo
zimeelekezwa kwenye barabara ambazo hazipitiki kabisa zipewe kipaumbele.





0 Maoni