Na mwandishi wetu

Makatibu Wakuu wa Wizara za Afya pamoja na Wataalam wa Wizara hizo kutoka Tanzania na Kenya wamekutana jana jijini Nairobi kujadili changamoto za masuala ya Corona kwa upande wa kibiashara upande wa mipakani mwa nchi hizo.

Mkutano huo ulitanguliwa na kikao cha awali cha wataalum wa sekta hiyo na baadae kufuatiwa na kikao cha Makatibu Wakuu hao ambao wamejadiliana masuala ya upimaji wa Corona baina ya nchi hizo mbili.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya Tanzania, Prof. Abel Makubi amesema mkutano huo ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo ya Marais wa nchi hizo mbili walipokutana mwaka huu jijini humo.

Ametaja baadhi ya mambo waliyoyajadili ni pamoja na kuhakikisha kunakuwa na mifumo inayoweza kuwasiliana katika upimaji kwa kuweza kuonekana kwa upande wa Tanzania na wakati huo huo kwa upande wa Kenya.

Kwa upande wa gharama za upimaji hususan kwa madereva wa magari makubwa, amesema wamejadili na kutoa mapendekezo yatakayopekekwa kwenye kikao cha Mawaziri wa nchi hizo mbili siku ya Alhamisi kupata maamuzi ya mwisho.

Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Kenya. Susan Mochache amesema wamejadili kurahisisha biashara kati ya nchi hizo mbili ikiwemo kupitisha mizigo tofauti ikiwemo chakula.