Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar imeitaka Wizara ya Biashara na Viwanda Zanzibar, kuweka bei elekezi katika baadhi ya bidhaa
muhimu ili kuepusha kuwaumiza wananchi hasa wa hali za chini.
Kauli
hiyo imetolewa na mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ambae
pia ni Makamo wa Pili wa Rais Zanzibar Hemed Suleiman Abdulla wakati akitolea
ufafanuzi malalamiko ya baadhi ya viongozi wa chama hicho walio kuwa wakiiomba
Serikali kuangalia upya suala la upandaji wa bei kwa baadhi ya bidhaa muhimu
ikiwemo mchele,unga na mafuta katika kikao Cha Viongozi na Wanachama wa CCM Mkoa
Mjini kilichofanyika katika ofisi za CCM Amani Agosti 8-2021
Mhe
Hemed amesema Serikali haitomvumilia mfanyabishara yoyote atakaekwenda kinyume
na bei elekezi zinazotolewa na Serikali na atakaebainika kutenda kosa hilo
atachukuliwa hatua kali za kisheria.
Katika
hatua nyengine Mhe Hemed amewaomba viongozi hao wa CCM kushirikiana na Serikali
katika kuunga mkono jitihada zinazochukuliwa katika mapambano dhidi ya Madawa
ya Kulevya ili kujenga Taifa lenye Afya bora na kupata viongozi bora wa
baadae.
Amesema
Serikali itachukua hatua kali ikiwemo kufanya marekebisho ya baadhi ya Sheria
kwa lengo la kuwadhibiti wale wote wanaojihusisha na vitendo haramu vya
kuharibu jamii ya wazanzibar.
Kwa
upande wake Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mjini Ndugu Talib Ali alimueleza Mjumbe
huyo wa Kamati kuu ya CCM Taifa kuwa katika uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020 kwa
mara ya kwanza Mkoa huo kuchukua ushindi wa majimbo yote kwa nafasi
zilizogombewa.





0 Maoni