Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akiwagiza watendaji wa kituo cha Damu salama kuwa makini katika kuzihifadhi damu hizo kutokana na tegemeo la kuokoa maisha ya wananchi

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imedhamiria kuimarisha utendaji kazi serikalini kwa kuwachukulia hatua watendaji wote wasio wajibuka ipasavyo katika majukumu yao ya kazi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla  ametoa kauli hiyo jana (August 10) alipofanya ziara ya kushtukiza katika kituo cha Damu salama kilichopo Sebleni Amani Kwa wazee.

Alileza kuwa, wapo watendaji wazembe wasiopenda kutekeleza majukumu katika sehemu zao za kazi jambo ambalo halileti ufanisi hivyo serikali itachukua hatua kwa lengo la kuimarisha utendaji katika kutoa huduma bora kwa wananchi.

Katika hatua nyengine Mhe Hemed amesema Kituo cha damu salama kina umuhimu mkubwa katika kuokoa maisha ya watu hivyo kuna kila sababu kwa watendaji wake kufanya kazi kwa uwadilifu na uwaminifu ili kufanikisha lengo lililokusudiwa.

Akikagua maabara maalum ya kuchunguza na kuhifadhia damu Makamu wa Pili wa Rais alimtaka msimamizi wa maabara hiyo kuwa makini katika kuhakikisha damu hizo zilizochangiwa kwa hiyari na wananchi zinahifadhiwa kwa umakini mkubwa.

Aidha, katika kuzipatia ufumbuzi changamoto zilizowasilishwa na wafanyakazi Mhe. Hemed alimtaka Mkurugenzi Mkuu wa Wiazra ya Afya Dk. Abdalla Suleiman kuzichukua changamoto hizo na kupitia uongozi wa Wizara ya Afya angalie namna bora ya kuzipatia ufumbuzi.

Pamoja na mambo mengine Makamu wa Pili wa Rais hakuridhishwa na utaratibu wa kuzihifadhi taka katika kituo hicho huku akimuagiza Mkurugenzi Mkuu huyo kuwasilisha taarifa kamili juu ya kuharibika kwa kifaa maalum cha Kuchomea taka ili kuepuka kuzaga kwa taka katika maeneo yasiokuwa rasmi.


Makamu wa Pili wa Rais akiwasili katika kituo cha Damu salama Amani Sbleni kwa Wazee kwa ajili ya kujionea mazingira ya utendaji kazi wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika kituo hicho.