Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania akishuka kwenye Ndege baada ya kuwasilia nchini Malawi kuhudhuria Mkutano wa SADC




 Na mwandishi wetu

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 16 Agosti, 2021 amewasili Lilongwe nchini Malawi kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 41 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) utakaofanyika tarehe 17 – 18 Agosti,2021.

Mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kamuzu, Mhe. Rais Samia amepokelewa na Mhe. Patricia Kaliati, Waziri wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii wa Malawi.

Katika Mkutano huo wa 41 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC, Jamhuri ya Malawi itathibitishwa kuwa Mwenyekiti wa SADC kwa kipindi cha mwaka mmoja (Agosti 2021 – Agosti 2022)

Aidha, Wakuu hao wa Nchi na Serikali watamthibitisha Katibu Mtendaji mpya wa SADC baada ya Katibu Mtendaji aliyepo Dkt. Stergomena Tax kumaliza muda wake baada ya kuhudumu kwa ufanisi nafasi hiyo kwa kipindi cha miaka nane.

Wakuu hao wa Nchi na Serikali wa SADC pia wanatarajiwa kujadili masuala mbalimbali ya Mtangamano pamoja na kuidhinisha kauli mbiu  ya Jumuiya hiyo.