Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akikata utepe kwa ajili ya kupokea rasmi Ambules iliyotolewa kwa ufadhili wa Benki ya NBC kwa ajili ya kutoa huduma katika Kijiji cha Kizimkazi kwenye Tamasha la Kizimkazi lililofanyika tarehe 28 Agosti 2021 katika Kijiji cha Kizimkazi Mkoa wa Kusini Unguja.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, ameitaka jamii nchini kulinda na kuendeleza mila, tamaduni na desturi zilizo nzuri na kuwarithisha vizazi vya sasa na vijazvyo.

Mhe. Rais Samia amesema hayo leo tarehe 28 Agosti, 2021 wakati akihutubia kwenye kilele cha Tamasha la Kizimkazi katika Kijiji cha Kizimkazi kusini Unguja Zanzibar.

Amesema kwa sasa dunia ipo kwenye zama za utandawazi hivyo mikakati thabiti inahitajika kuhakikisha jamii inalinda mila, tamaduni na desturi zilizo nzuri ili zisipotee na kuachana na zile mbaya kama ndoa za utotoni na ukeketaji.

Mhe. Rais Samia amesema pamoja na mambo mengine, Tamasha la Kizimkazi linahamasisha miradi ya maendeleo kufanyika ikiwemo ujenzi na ukarabati wa shule za awali, Msingi na Sekondari, nyumba za walimu pamoja na nyumba za watumishi wa afya.

Lengo jingine la Tamasha hilo ni kutangaza fursa za kiuchumi zilizopo kwenye eneo hilo hususan kilimo, utalii, uchumi wa bahari ama uchumi wa buluu na utalii wa pomboo (Dolphin) ambao hupatikana katika eneo hilo la Kizimkazi.

Vilevile, Mhe. Rais Samia amewahimiza wananchi kushiriki kikamilifu kwenye zoezi la Sensa linalotarajiwa kufanyika mwezi Agosti mwaka 2022, kwa kuwa Sensa ni muhimu katika kuwezesha Serikali kufahamu idadi ya watu itakayosadia kupanga mipango ya maendeleo.

Mhe. Rais Samia amewataka wananchi kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya UVIKO 19 na kujitokeza kupata chanjo katika kukabiliana na maradhi hayo.

Katika kilele cha Tamasha hilo Mhe. Rais Samia ametembelea mabanda ya Wajasiriamali na kujionea bidhaa wanazozalisha, kuzindua majengo mbalimbali, kupokea maandamano ya vijana takribani 250 na kushuhudia maonesho ya asili ya Shomoo. 

Mhe. Rais Samia amewashukuru wafadhili waliochangia miradi ya maendeleo na  kufanikisha kufanyika kwa Tamasha hilo ikiwemo Benki ya CRDB, NMB, NBC, Kampuni na Mshirika mbalimbali pamoja na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akiondoa kitambaa kuzindua rasmi Nyumba za Madaktari na Jengo la Ofisi ya Maendeleo Kizimkazi katika Tamsha la Kizimkazi zilililofanyika leo tarehe 28 Agosti 2021 katika Kijiji cha Kizimkazi Mkoa wa Kusini Unguja.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akifurahia mashindano ya mchezo wa kuvuta Kamba kati ya Timu za Vijana Wanawake na Wanaume katika Kijiji cha Kizimkazi, kwenye  Tamasha la kizimkazi lililofanyika tarehe 28 Agosti 2021 katika Kijiji cha Kizimkazi Mkoa wa Kusini Unguja.