Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamehitimisha Mkutano wa 41 wa Kawaida wa Jumuiya hiyo uliofayika kwa siku mbili Lilongwe nchini Malawi.
Katika siku ya pili na
ya mwisho ya Mkutano huo, Wakuu hao wamesani nyaraka za kisheria 4 ambazo ni Itifaki ya Takwimu, Mkataba wa
Marekebisho ya Itifaki ya Nishati ya SADC na Marekebishio ya Kiambatisho Na.1
cha Itifaki ya Nishati ya SADC, Mkataba wa kuboresha Itifaki ya SADC ya Silaha
na Mkataba kuhusu hadhi ya Jeshi la dharura la SADC.
Akisoma tamko la
pamoja, Katibu Mtendaji anayemaliza muda wake Dkt. Stergomena Tax amesema Wakuu
hao wa Nchi na Serikali wamemthibitisha na kumuapisha Katibu Mtendaji mpya wa
Sekretarieti ya Jumuiya hiyo Bw. Elias Mpedi Magosi kutoka Jamhuri ya Botswana
ambaye anakuwa Katibu Mtendaji wa 7 baada ya aliyekuwa Katibu Mtendaji Dkt. Stergomena Tax kumaliza muda wake wa
miaka 8 ya utendaji katika SADC.
Dkt. Tax ameongeza kuwa
Wakuu hao wa Nchi na Serikali wameendelea kusisitiza kuondolewa kwa vikwazo vya
Kiuchumi dhidi ya Zimbabwe bila masharti na kuiunga mkono Zimbabwe kwa jitihada
zake za kuendelea kuimarisha uchumi wake.
Vilevile, Wakuu hao wa
Nchi na Serikali wamewapongeza Wananchi na Serikali ya Jamhuri ya Zambia kwa
kufanya uchaguzi Mkuu na kumpongeza Rais Mteule Mhe. Hakainde Hichilema kwa
kuibuka mshindi.
Viongozi hao wa SADC
wamepokea taarifa kuhusu hali ya Usalama katika jimbo la Cabo Delgado Kaskazini
mwa Msumbiji na kupongeza Nchi wanachama wa SADC kwa michango yao ya kifedha
iliyowezesha kupelekwa kwa Jeshi la Dharura la SADC nchini Msumbiji.
Mkutano huo wa 41 pia
umeridhia mabadiliko ya Jukwaa la Bunge la SADC kuwa Bunge la SADC la ushauri
na majadiliano.
Dkt. Tax amesema Wakuu
hao wa Nchi na Serikali wa SADC kwa kauli moja wamekubaliana kuwa Mkutano wa 42
wa Kawaida wa Jumuiya hiyo utafanyika
nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Agosti 2022.
Nje ya Mkutano huo,
Mhe. Rais Samia amekutana na kufanya mazungumzo na Rais mstaafu wa Malawi
Mhe. Joyce Banda.
Mhe. Rais Mstaafu Joyce
Banda amempa pole Mhe. Rais Samia kufuatia msiba wa Hayati Rais Magufuli na
kumpongeza kwa kushika nafasi ya Urais, ambapo amemuahidi kumpa ushirikiano
akiwa Rais mstaafu mwanamke.
Kwa upande wake Mhe.
Rais Samia amemshukuru Rais Mstaafu Banda na kuahidi kuendeleza ushirikiano wa
kidugu na wa kihistoria kati ya Tanzania na Malawi.




0 Maoni