Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akisalimiana na kumpongeza Rais Mpya wa Zambia Mhe. Hakainde Hichilema, mara baada ya kuapishwa kuwa Rais wa 7 wa Zambia katika Uwanja wa Taifa wa Mashujaa (National Heroes Stadium) Jijini Lusaka Zambia leo Agosti 24,2021.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 24 Agosti, 2021 amehudhuria sherehe za kuapishwa kwa Rais wa Saba wa Zambia Mhe. Hakainde Hichilema zilizofanyika katika Uwanja wa Taifa wa Mashujaa (National Heroes Stadium), Jijini Lusaka.

 Mhe. Rais Samia amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Hichilema ambapo amempongeza kwa ushindi wa nafasi ya Urais pamoja na kuwapongeza wananchi wa Zambia kwa kufanya uchaguzi wa amani. Mbali na salamu za pongezi amemuahidi Rais Hichilema kuendeleza ushirikiano na uhusiano wa kihistoria uliopo baina ya Tanzania na Zambia.

 Katika mazungumzo hayo Mhe. Rais Samia na Mhe. Rais Hichilema wamezungumzia umuhimu wa kuihuisha mikutano ya Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) ili kuweza kubaini fursa mbalimbali za ushirikiano ikiwemo kuimarisha ushirikiano uliopo wa  Shirika la Reli la Tanzania na Zambia (TAZARA) na Bomba la mafuta la Tanzania na Zambia (TAZAMA).

 Lengo la mikutano hii mbali na kuibua fursa mbalimbali pia ni kuweza kutatua changamoto ziliopo katika sekta mbalimbali ili ziweze kuwa na tija na kutoa  manufaa kwa  nchi mbili hizo.

 Mhe. Rais Samia ameeleza umuhimu wa kukuza biashara baina ya Tanzania na Zambia ili uende sambamba na uhusiano wa kihistoria tuliokuwa nao.  Mhe. Rais Samia ameiomba Serikali ya  Zambia kuendelea kutumia Bandari ya Dar es Salaam kupitishia mizigo yake, ombi ambalo lilikubaliwa na kuungwa mkono na Mhe. Hichilema.

 Kwa upande wake Mhe. Rais Hichilema ametoa salamu za rambirambi kwa Mhe. Rais Samia na Watanzania wote kwa kumpoteza Hayati Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 Aidha, Mhe. Rais Hichilema amemshukuru Mhe. Rais Samia kwa kushiriki katika sherehe za uapisho na kuahidi kufanya kazi na nchi zote jirani na utayari wake wa kushirikiana na nchi hizo katika kudumisha urafiki wa kidugu na kihistoria kwa maendeleo ya wananchi wake. 

 Mhe. Rais Hichilema mesisitiza umuhimu wa kukuza biashara kama njia ya  kujenga uchumi wa nchi yake na kuinua maisha ya wananchi wake. Vilevile alizungumzia umuhimu wa Tume za Pamoja za Kudumu za Ushirikiano hususani kwenye suala zima la kushughulikia changamoto zinazokwamisha ushirikiano ambapo ameahidi kutoa msukumo wa kisiasa kuhakikisha mikutano hiyo inafanyika mara kwa mara.

 Vilevile, Mhe. Rais Hichilema amemshukuru Mhe. Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Kikwete kwa kazi nzuri aliyoifanya na uongozi uliotukuka katika kusimamia timu ya Waangalizi wa Uchaguzi kutoka  Jumuiya ya Madola  na ameeleza kuwa yeye kama kiongozi mgeni yupo tayari kujifunza kwa viongozi wakongwe.

 Katika hatua nyingine, Mhe. Rais Samia amemualika Mhe. Rais Hichilema kufanya ziara  Nchini Tanzania, na Mhe. Rais Hichilema amekubali mwaliko huo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akiszungumza na Rais Mpya wa Zambia Mhe. Hakainde Hichilema, mara baada ya kuapishwa kuwa Rais wa 7 wa Zambia katika Uwanja wa Taifa wa Mashujaa (National Heroes Stadium) Jijini Lusaka Zambia leo Agosti 24,2021