Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia
Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Oman nchini
Balozi Ali Bin Abdallah Bin Salim Al
Mahrouqi aliyemaliza muda wake wa uwakilishi hapa nchini.
Katika mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Dodoma, Balozi
Al Mahrouqi amempongeza Rais Samia kwa utawala wake na kuishukuru Serikali ya
Tanzania kwa ushirikiano mkubwa
alioupata wakati alipokuwa akitekeleza majukumu yake.
Amesema Tanzania na Oman zina uhusiano mzuri na wa
muda mrefu hivyo kuomba kuendelezwa kwa ajili ya maslahi ya nchi zote mbili
pamoja na kuimarishwa biashara.
Nae Rais Samia amemhakikishia Balozi Al Mahrouqi
kuwa Tanzania itaendeleza na kudumisha ushirikiano wake na Oman kwa maslahi ya
nchi zote mbili.
Amemjulisha Balozi huyo kuwa kwa sasa Tanzania
inapitia sheria na sera zake mbalimbali za biashara ili kujenga mazingira
mazuri zaidi ya biashara na uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuongeza ufanisi katika viwanja vya Ndege na
Bandari ili kurahisisha ufanyaji biashara baina ya nchi hizi mbili.
Pia, Rais amezitaka Tume za pamoja kati ya Tanzania
na Oman kukutana na kuzungumza ili kuimarisha mambo mbalimbali baina ya nchi
hizo.
Rais Samia amemshukuru na kumpongeza Balozi Al Mahrouqi kwa kazi nzuri ya uwakilishi wake hapa nchini katika kipindi cha miaka 4 kwa kudumisha uhusiano kati ya Oman na Tanzania.







0 Maoni