Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan (katikati) akifurahi  pamoja na baadhi ya  viongozi waandamizi wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar na viongozi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) mara baada ya kuzindua  Kliniki inayohamishika (mobile Clinic) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa serikali ya Mapinduzi ya Waziri wa Afya Ahmed Nassor Mazrui (wa pili kushoto), Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Katiba na Sheria, Haroun Ali Suleiman (Kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa tatu kushoto) na Mkurugenzi wa wateja binafsi wa benki hiyo Bw Elibariki Masuke  (Kushoto).
Wanafunzi na wakazi wa Kijiji cha Kizimkazi Mkunguni Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar wakiwa wameketi pembeni ya Kliniki inayohamishika (mobile Clinic) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuboresha huduma ya afya hususani ya mama na mtoto visiwani humo wakati wa hafla ya makabidhiano iliyofanyika leo Kijiji cha Kizimkazi Mkunguni Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar

Na Mwandishi wetu

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameishukuru Benki ya Biashara ya NBC kwa jitihada wanazozifanya katika kuunga mkono  serikali kwa kuchangia katika kuboresha na kuimarisha Miradi ya Kimaendeleo inayowagusa wananchi.

 Raisi Samia ameyasema hayo Jana Agost 28 katika uzinduzi na makabidhiano ya Kliniki inayohamishika (mobile Clinic) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuboresha huduma ya afya hususani ya mama na mtoto visiwani sambamba na kuzindua jengo la madarasa ya skuli ya  maandalizi ya Kizimkazi yaliyojengwa na kukarabatiwa kwa msaada kutoka Benki hiyo.

Katika hatua nyengine Rais Samia ametoa wito kwa taasisi hiyo pamoja na taasisi nyingine za kifedha kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuleta maendeleo kwa wananchi wake.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi alisema msaada huo wenye  jumla ya thamani ya Tsh Milioni 275, ni muendelezo wa jitihada za benki hiyo za uwajibikaji kwa jamii (CSR)zinazosukumwa na dhamira kuu ya taasisi hiyo katika kushirikiana na jamii inayoihudumia.

“Benki ya NBC tumekuwa tukiguswa na changamoto mbalimbali zilizopo kwenye huduma za afya na elimu hapa nchini ikiwemo Zanzibar na ndio maana tumekuwa mstari wa mbele kuhakikisha tunashirikiana na serikali zote mbili kukabiliana na changamoto zinazohusu sekta hii muhimu.’’ Alisema huku akibainisha kuwa benki hiyo inaendelea kufanya jitihada zaidi ili kufanikisha misaada  kama hiyo kwenye maeneo mengine ikiwemo visiwani Pemba.

Alisema huduma zitakazotolewa na kliniki hiyo kwa akina mama na watoto zitatolewa bure kwa kuwa zitagharamiwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar .

“Pamoja na msaada huu benki ya NBC itaendelea kuhudumia vifaa vilivyopo ndani ya kliniki hii hata pale vitakapokuwa vinapata hitirafu za kiufundi. Tunaamini sasa kupitia huduma hii wataalamu wa afya wataweza kuwafikia walengwa popote walipo hususani wale waliopo pembezoni hususani wakina mama na watoto na kupitia msaada wa mwenyezi Mungu tutaweza kuokoa maisha yao,’’ aliongeza.

Mbali na ujenzi wa jengo la Madarasa katika wa skuli ya maandalizi Kizimkazi msaada huo pia umehusisha samani za ndani ya madarasa hayo ikiwemo madawati na meza sambamba na jiko kwa ajili ya upishi wa chakula cha wanafunzi hao pamoja na vifaa vya michezo ili kutoa fursa ya watoto kufurahia michezo yao.

Hafla ya makabidhiano hayo imefanyika Kijiji cha Kizimkazi Mkunguni Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar na kuhudhuriwa na baadhi ya  viongozi waandamizi wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar, akiwemo Waziri wa Afya Zazibar, Ahmed Nassor Mazrui, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Katiba Sheria, Utumishi na Utawala Bora wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Haroun Ali Suleiman, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Rashid Hadid Rashid, viongozi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC)na wananchi wa kijiji hicho.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (kulia) akifafanua jambo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan  wakati Rais alipokuwa akigagua jengo la madarasa ya Skuli ya  Maandalizi ya Kizimkazi lililojengwa na kukarabatiwa kwa msaada wa benki ya NBC
Monekano wa jengo la madarasa ya Skuli ya  Maandalizi ya Kizimkazi lililojengwa na kukarabatiwa kwa msaada wa benki ya NBC.

Baadhi ya wagenini waalikwa pamoja viongozi wa benki ya NBC wakifuatilia makabidhiano hayo.

Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa NBC, Neema Rose Singo (Kulia) akimkabidhi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan  zawadi kwa niaba ya Umoja wa wanawake wa benki hiyo ikiwa ni ishara ya kumpongeza na kutambua jitihada za Rais Samia katika kuliongoza taifa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan (katikati) akifurahia  pamoja na baadhi ya  viongozi waandamizi wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar na viongozi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) mara baada ya kuzindua jengo la madarasa ya Skuli ya  Maandalizi ya Kizimkazi lililojengwa na kukarabatiwa kwa msaada wa benki ya NBC