Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake
watatu wamesomewa upya mashtaka sita yakiwemo ya kufadhili vitendo vya ugaidi
na kukusanya pesa za kufanya vitendo hivyo.
Mashtaka mengine ni kukutwa na silaha aina ya
bastola na kukutwa na sare za jeshi kinyume cha sheria.
Kati ya mashtaka hayo sita, Mbowe anakabiliwa na
mashtaka mawili ambayo ni kula njama na kufadhili fedha kwa ajili vitendo vya
kigaidi.
Mshtakiwa Mbowe na wenzake watatu wamesomewa upya
mashtaka yao hii leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba ambayo ni kula
njama na tuhuma za Ugaidi ambayo waliyatenda kati ya Mei 1 na August 1, 2020
maeneo ya Moshi, Dar es Salaam, Morogoro na Arusha.
Mbali na Mbowe, ambaye ni mshtakiwa wa nne katika
kesi hiyo, washtakiwa wengine ni Halfan Hassa, Adam Kasekwa na Mohammed
Lingwenya.
Washtakiwa baada ya kusomewa amshtaka hayo hawakutakiwa
kujibu chochote ambapo Hakimu Simba ameahirisha kesi hiyo hadi Agosti 13, 2021
itakapotajwa.
Washtakiwa hao wanaotetewa na jopo la mawakili tisa
wakiongozwa na Peter Kibatala wamerudishwa rumande, kwakuwa mashtaka
yanayowakabili hayana dhamana kwa mujibu wa sheria.





0 Maoni