Mwonekano wa gari lililokuwa limewabeba maofisa wadhamini na kupata nayo ajali katika eneo la Pandani Pemba
 

Na Mwandishi wetu

Maofisa wadhamini  Watatu wamenusurika kifo baada ya kutokea ajali ya gari  asubuhi ya leo Agosti 30 katika eneo la Pandani skuli, Shehia ya Pandani, Wilaya ya Wete,  Mkoa wa Kaskazini Pemba baada ya gari walilokua wakisafiria  kupoteza mwelekeo kutokana na kupasuka kwa gurudumu la mbele.

 Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Mkuu wa Wilaya ya Wete Mgeni Khatib Yahya  ambae alikua katika eneo la tukio amesema ndani ya gari hiyo iliyopata ajali ilikuwa inajumla ya watu wanne, maofisa wadhamini watatu na dereva aliekuwa akiendesha gari hilo ila wote wamefanikiwa kutoka salama

 Mhe Mgeni amesema baada ya ajali hiyo,  majeruhi wote waliwahishwa katika Hospitali ya Micheweni kwaajili ya uchunguzi zaidi na baada ya Vipimo wote walionekana wazima  na majira ya saa saba za mchana waliruhusiwa kurudi nyumbani.

 waliojeruhiwa katika ajali hiyo  ni Ahmed Abubakar Mohamedi ambae ni Afisa mdhamini Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Raisi, wengine ni Aly Salum Mata Afisa mdhamini Ofisi ya Raisi, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za Smz na Abdulwahab Bakari ambae ni Afisa Mdhamini Wizara ya Fedha na Mipango na Dereva wa gari hili ambae jina lake hatukulipata.

 Wakizungumza na sknews wananchi walioshuhudia tukio hilo wamesema maeneo ya Pandani skuli  sio salama kwakua pamekua pakitokea ajali za mara kwa mara na wao wamekua wakizishuhudia bila kujua sababu ya eneo hilo kutokea ajali nyingi.