Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge imemtia hatiani Mbunge wa Kawe, Askofu Josephat Gwajima kwa makosa ya kudhalilisha na kushushsa nafasi ya Bunge, wabunge na viongozi, kuchonganisha mhimili wa bunge dhidi ya mhimili wa serikali na wananchi na kuonesha dharau na kushusha heshima ya bunge, shughuli za bunge na uongozi wa bunge.

Akizungumza bungeni Jijini Dodoma hii leo Mwenyekiti wa Kamati ya haki, maadili na madaraka ya bunge Emmanuel Mwakasaka, amesema kuwa mbunge Josephat Gwajima amekutwa na hatia baada ya Kamati ya maadili kumuhoji juu ya shutuma zinazomkabili na kisha kukiri kuwa maneno aliyoyatoa ni ya kwake mwenyewe na kwamba alikuwa akiwahubiria waumini wake ulimwenguni kote kuhusiana na janga la Covid-19 na chanjo ambazo zinatolewa

Baada ya kumtia hatiani, kamati hiyo imeazimia Askofu Gwajima apewe adhabu ya kutohudhuria mikutano miwili ya Bunge.

Itakumbukwa kuwa Gwajima amekuwa akitumia Kanisa lake la Ufufuo na Uzima kwa kuikosoa serikali ya Tanzania kuhusu chanjo ya Corona zinazoendelea kupigwa nchini kwa kile alichodai kuwa chanjo hiyo ni nia mbaya ya Mataifa ya magharib kwa Tanzania, huku akionekana kwenda kinyume na Rais wa nchi na viongozi wengi wa serikali katika uhamasishaji wa uchomaji chanjo hiyo.