Imamu mkuu wa Ghana, Shehe Osman Sharubutu amechangia zaidi ya $8,000 (£5,800) ili kusaidia ujenzi wa kanisa kuu la kitaifa lenye utata.

Taifa hilo lina historia ya kuwa na mahusiano mazuri ya amani ingawa hatua ya kiongozi wa dini kuchangia fedha nyingi kwa imani nyingine si jambo la kawaida.

Imamu mwenye umri wa miaka 102-amesema ameamua kufanya jambo hilo ili kuimarisha amani ambayo ipo kati ya wakristo na waislamu.

Miaka miwili iliyopita kiongozi huyo alihudhuria ibada ya Pasaka katika kanisa katoliki na kusababisha gumzo kwenye mitandao ya kijamii.

Kwa sasa serikali imezindua ujenzi wa kanisa na kuwasisitiza Waghana wachangie katika ujenzi huo, kanisa hilo linajengwa katika mji mkuu wa Accra, na gharama za ujenzi zinatarajiwa kuwa zaidi ya dola milioni 100.

Ujenzi wa kanisa hilo la taifa unatarajiwa kumalizika mwaka 2024, ikijumuisha na makumbusho ya biblia na ukumbi unaoenea viti 5,000.