Msimamizi wa Chanjo ya Kipindupindu Unguja
Dkt. Fadhil Mohammed Abdalla akielezea azma ya serikali juu ya Chanjo ya
kipindupindu pamoja na umuhimu wa Chanjo hiyo katika mafunzo kwa Waandishi wa
habari yaliyofanyika Ukumbi wa Sanaa Rahaleo Mjini Unguja.Na mwandishi wetu
Msimamizi wa Chanjo ya Kipindupindu Unguja Dkt.
Fadhil Moh’d amesema chanjo ya kipindupindu haina mahusiano na chanjo ya Corona
na haina madhara yoyote kwa binadamu.
Ameyasema hayo kwenye Ukumbi wa Sanaa Rahaleo wakati
alipokuwa akitoa mafunzo kwa Waandishi wa Habari kuhusu Umuhimu wa kumaliza
Dozi ya Pili ya chanjo hiyo.
Ameeleza kuwa azma ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
juu ya chanjo ya Kipindupindu inayotolewa kwa njia ya matone ni kutokomeza
kabisa ugonjwa huo nchini hivyo amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika
zoezi hilo.
Aidha Dk. Fadhili amewasihi wananchi kuachana na
uvumi kuhusu usalama wa chanjo hiyo, amesema ni salama.
Akiwasilisha mada kuhusu Umuhimu wa Chanjo ya
kipindupindu Dozi ya Pili Mkuu wa
Kitengo cha Elimu ya Afya, Halima Khamis amesema atakaemaliza dozi kamili ya
chanjo hiyo ataepukana na ugonjwa huo kwa muda mrefu.
Amewataka wananchi kuendelea kufuata kanuni za
kujikinga na maradhi ya kipindupindu ili kuhakikisha Zanzibar inatokomeza kabisa
ugonjwa huo.
Hata hivyo amewasisitiza waandishi wa habari kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi katika awamu ya pili ya chanjo ya kipindupindu ambayo imeanza kutolewa jana hadi 11/08/2021.




0 Maoni