Mtu mmoja ameuawa kwa kupigwa risasi wakati wakaazi
wa Kianjokoma huko Embu, kati mwa Kenya walipofanya maandamano juu ya kifo cha
ndugu wawili mikononi mwa polisi.
Kwa siku mbili, wakaazi wa eneo hilo walifunga
barabara na kutaka haki kwa familia ya Benson Njiru (22) na mdogo wake,
Emmanuel Mutura (19).
Wawili hao walikamatwa katika mji wa Kianjokoma
Jumapili usiku kwa madai ya kuwa nje kipindi cha marufuku ya kutoka nje cha saa
nne usiku.
Familia yao imesema baada ya kuwatafuta katika vituo
vya polisi vya karibu na eneo lao, bila matokeo, walipata miili yao katika
chumba cha kuhifadhi maiti cha hospitali kuu ya Embu.
Polisi wanadai wawili hao waliruka kutoka kwa gari
la polisi lililokuwa mbioni.
Mamlaka Huru ya Uangalizi wa Polisi (IPOA) imesema
inachunguza vifo hivyo na imetuma maafisa wake katika eneo hilo. Mamlaka hiyo
imeelezea wasi wasi kwamba vifo hivyo sio vya kwanza vinavyotokana na
utekelezaji wa masharti ya Covid.
Makundi ya kutetea haki za binadamu yamekuwa yakilalamikia mauaji kadhaa ya kiholela nchini Kenya, mengine ambayo hayajatatuliwa kwa miaka. Ni maafisa wachache tu wa polisi ambao wamewahi kushtakiwa.





0 Maoni