Balozi Mdogo wa China Bw. Zhang Zhisheng akimkabidhi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Stakabadhi ya makabidhiano ya mdaada wa Chanjo ya Covid- 19 inayotarajiwa kukabidhiwa baada ya kuwasili Zanzibar.

Zanzibar

Jumla ya chanjo laki moja (100,000) zinatarajiwa kukabidhiwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwa ni msaada kutoka Serikali ya Jamhuri ya watu wa China.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla alieleza hayo Ofisini kwake Vuga Jijini Zanzibar wakati akipokea Stakabadhi ya msaada huo wa chanjo kutoka kwa Balozi Mdogo wa China anaefanyia kazi zake Zanzibar Bwana Zhang Zhisheng

Mhe. Hemed alisema chanjo hizo aina ya SINOVAC zinategemewa kuwasili Zanzibar ndani ya muda mfupi baada ya kupokea Stakabadhi na mara baada ya kuwasili Zanzibar zinatakibidhiwa kwa Wizara ya Afya ikiwa ndio wizara yenye dhamana na musuala ya Afya.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itapokea chanjo hizo, ikiwa ni katika juhudi za kujikinga na Maradhi ya Covid 19, kwa lengo la kuwakinga wananchi wake kutokana na virusi vinavyosababisha maradhi hayo.

Akizungumzia Ubora wa chanjo hiyo Makamu wa Pili wa Rais aliwahakikishia wananchi wa Zanzibar kuwa chanjo hiyo ni salama kwani imethibitishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa ajili ya matumizi.

Katika hatua nyengine Mhe. Hemed aliendelea kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya watu wa China kwa kuendelea kuunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hasa katika Sekta ya Afya, akitolea mfano misaada mbali mbali inayotolewa na Nchi hiyo katika Hospitali na Mnazi Mmoja na ya Hospital ya Abdallah Mzee kwa Upande wa Pemba.

Alifafanua kuwa, mashirikiano hayo yanaonesha ukaribu na udugu kati ya nchi hizo mbili yaliyoasisiwa kwa muda mrefu sasa ambapo hadi sasa China na Zanzibar zinashirikiana kupitia sekta tofauti.

Nae Balozi Mdogo wa China Bwana Zhang Zhisheng alisema China imejipanga kutoa chanjo ili kusaidia kinga dhidi ya covid 19 na alimuhakikishia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa chanjo hizo ni salama kutokana na kupatikana kwa ruhusa ya kimatumizi kutoka  Shirika la Afya Duniani (WHO).

Aidha, Bwana Zhang Zhisheng alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa Nchi ya China itaendeleza mashirikiano yaliyopo baina yao ili kuisaidia  Zanzibar kukuza uchumi wake ambapo serikali ya Jamuhuri ya watu wa China imejipanga kuisaidia Zanzibar katika kuwekeza kwenye Sekta ya Viwanda jambo ambalo litasadia kuinua uchumi wa zanzibar na watu wake.

Balozi mdogo wa China Bw. Zhang Zhisheng akimueleza Mhe. Hemed juu ya ubora wa Chanjo aina ya SINOVAC iliotolewa na serikali ya Jamuhuri ya watu wa China kuwa ipo salama na imethibitishwa na Shirika la Afya Duniani(WHO).

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akimshkuru Balozo mdogo wa China aliefika Afisini kwake Vuga kwa ajili kumkabidhi Stakabadi za msaada wa Chanjo zilizotolewa na Nchi Hiyo ya China.