Wananchi wa kijiji cha Paris kilichopo Wilaya ya Kati Mkoa wa KusiniUnguja, Visiwani Zanzibar, wametakiwa kuwafichua wahalifu  wanaopatikana katika maeneo yao ili waweza kuishi kwa amani na utulivu.

Hayo yamesemwa leo na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Khamis Hamza Chilo wakati akizungumza na wananchi wa Kijiji hicho kwenye Mkutano wa Hadhara wakati wa ziara yake yakuendelea kuskiliza Changamoto mbali mbali zinazowakabili wananchi

Amwataka wananchi hao kuungana na Serikali katika kuhakikisha wale wote wanaojihusishwa na matukio ya Uuzaji na utumiaji wa dawa za kulevya,matendo ya udhalilishaji,uporaji na wizi wanaripotiwa katika vyombo vya Sheria.

“Kuna wengine wamesema yapo matukio ya kihalifu hapa yanafanyika, watu wanaiba hapa, watu wanatembea uchi, bangi zinauzwa hapa, sasa akitokea mtu anatokea sehemu ya mbali kama mlivyosema  anafanya matendo ya uhalifu basi mripoti kwa Jeshi la Polisi,mkishajua huyu ndio muuza unga maarufu hata mimi niambieni nitawatuma askari wangu waje wamshughulikie,msimpige wala msichukue sheria mkononi chukueni hatua za kinidhamu na kisheria sio mumpige mtakuja kutengeneza balaa linguine” alisema Naibu Waziri Chilo

Awali mkazi wa Kijiji hicho Said Mpangaleni akizungumza  katika mkutano huo amesema kuwepo kwa uhalifu uliokithiri katika Kijiji chao imepelekea  kudumaa kwa shughuli za kimaendeleo watu wakihofia usalama wao

“Hapa kuna genge la uuzaji na utumiaji dawa za kulevya na ndio linaratibu uhalifu wote katika Kijiji hiki,mtu akishakula maunga yake kinachofatia ni uhalifu tu kwa kweli tumekua tukiishi kwa hofu,bora sisi wanaume tuna afadhali lakini dada zetu wanaporwa mchana kweupe,Serikali itusaidie kwenye hili kwani kwa hali hii huo uchumi tunaoambiwa hatuwezi kuupata hali huku ni tete” alisema Said

Wakitoa neno la shukrani baada ya mkutano huo wawakilishi wa wananchi hao wameiomba serikali kufungua kituo cha polisi katika maeneo hayo kwani itarahisisha udhibiti wa uhalifu katika Kijiji chao hali itakayopelekea kustawi kwa amani huku pia wakiomba kuongezwa kwa askari wa ulinzi shirikishi.