Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 07 Julai, 2021 ameanza ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Mororogo.

 Akiwa katika eneo la Kibaigwa Mkoani Dodoma njiani kuelekea mkoani Morogoro, Mhe. Rais Samia amewataka wananchi wa eneo hilo na Watanzania kwa ujumla kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Corona kwa kufuata maelekezo ya wataalam wa Afya ili kuepuka kupata maambuzi ya ugonjwa huo.

 Mhe. Rais Samia amesema baadhi ya maeneo nchini tayari yana wagonjwa wa Corona hivyo ni vyema wananchi wakafuata maelekezo ya wataalam wa Afya ikiwa ni pamoja na kuvaa barakoa ili waweze kujikinga na maambukizi ya ugonjwa huo.

 Katika eneo la Msamvu mkoani Morogoro, Mhe. Rais Samia amewasihi wakazi wa mkoa huo pamoja na wananchi wengine kuendelea kuitunza amani iliyopo nchini kwasababu ndio msingi mkuu wa maendeleo ya taifa lolote duniani.

“ kuna baadhi ya watu wameshaanza chokochoko naomba muwapuuze kwani hawawatakii mema, wanataka kuvunja amani ya nchi iliyopo kwa muda mrefu na kusababisha vurugu nchini” . amesema Mhe. Rais Samia.

 Pia Mhe. Rais Samia amewapongeza wakazi wa mkoa wa Morogoro kwa kuwa sehemu ya miradi mikubwa miwili ya kimkakati ya Reli ya Kisasa (SGR) na Mradi wa Kufua Umeme wa Mwalimu Nyerere katika mto Rufiji.

 Amesema kutokana na kuwepo kwa miradi hiyo mkoani Morogoro ni vyema wananchi wakawa walinzi ili iweze kuwanufaisha wao na taifa kwa ujumla.

 Aidha, Mhe. Rais Samia amewahakikishia wakazi wa mkoa wa Morogoro kuwa changamoto mbalimbali zinazowakabili zikiwemo uhaba wa maji, migogoro ya ardhi, masuala ya afya na mengineyo kuwa serikali tayari imeshazifanyia kazi.

 Kesho tarehe 8 Julai, 2021 Mhe. Rais Samia ataendelea na ziara yake mkoani Morogoro ambapo atashiriki mkutano mkuu wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT).