Mkuu wa Wilaya ya Ubungo  Mheshimiwa Kheri James ametolea maamuzi mgogoro wa  ardhi wa eneo la Goba –Kisauke  katika mtaa wa Tegeta A uliodumu kwa muda wa miaka   mitano na kuelekeza kuwa eneo hilo libaki kuwa  mali ya Mtaa (kijiji).

 Akuzungumza na wananchi wa  Mtaa huo  wakati wa mkutano wa hadhara wa kutole maamuzi mgogoro huo  leo julai 19, 2021, alisema maamuzi  hayo yametolewa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi baada ya kufanya uchunguzi wa madai yaliyowasilishwa na familia Tabia Mziwanda na Roman Mosha.

 Alisema Tume ya uchunguzi iliyoundwa na serikali kuchunguza mgogoro huo ilibaini kuwa familia ya Tabia  Mziwanda  ambayo ilikuwa ikidai kuwa eneo hilo ni mali yao haikuwa nyaraka zozote zinazo halalisha umiliki wa eneo hilo.

 Aliongeza kuwa Tume ilibaini   Bwana Roman Mosha aliuziwa eneo lenye ukubwa ekari nne na  kamati ya kijiji kwa kipindi hicho  kinyume na taratibu za kuuza ardhi ya vijiji inayotaka uuzwaji wa ardhi uridhiwe kwenye Mkutano Mkuu wa Kijiji na si kamati.

 ‘’Bwana Mosha alileta mkataba wa   mauziano ya ardhi baina yake na kijiji, ambayo inaonesha aliuziwa ekari nne, na katika kamati hiyo mmoja wao ni Mzee mziwanda ambae familia yake inadai kuwa eneo hilo ni mali yao,  serikali imejiridhisha na ushahidi wote uliotolewa na kamati ya uchunguzi kuwa hakuwahi kuwa mmliki wa eneo hilo’’alisema.

 Kheri alisema kuwa baada ya Serikali kushirikiki kamilifu katika kuchunguza mgogoro huo na kusikiliza pande zote mbili kihistoria, kimazingira, kinyaraka, viongozi wa Mtaa, na wazee wa Mtaa huo serikali imetoa maamuzi kuwa eneo hilo litabaki kuwa mali ya kijiji (mtaa),na kusimamiwa na Halmashauri ya Manispaa ya ubungo kama sheria ya ardhi inavyoelekeza.

 Aliwataka viongozi wa Mitaa kuacha kuuza ardhi kiholela na badala yake  kufuata  taratibu   za kuuza ardhi katika maeneo yao ili kuepusha  migogoro  mbalimbali ya ardhi inayojitiokeza   na kuathiri shughuli mbalimbali za maendeleo.

 ’’Hakikisheni mnalilinda eneo hili,  mtakapotaka kufanya matumizi mfuate taratibu,  babu zetu walitenga maeneo haya kwaajili ya  kupanua maendeleo  ya mitaa  kama vile kujenga shule, Vituo vya afya, na miradi mingine ya maendeleo hivyo yalindeni  maeneo haya’’