Mkuu wa Wilaya ya
Ubungo Mheshimiwa Kheri James ametolea maamuzi mgogoro wa ardhi wa
eneo la Goba –Kisauke katika mtaa wa Tegeta A uliodumu kwa muda wa
miaka mitano na kuelekeza kuwa eneo hilo libaki kuwa mali ya
Mtaa (kijiji).
Akuzungumza na wananchi wa Mtaa huo wakati wa mkutano wa hadhara wa kutole maamuzi mgogoro huo leo julai 19, 2021, alisema maamuzi hayo yametolewa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi baada ya kufanya uchunguzi wa madai yaliyowasilishwa na familia Tabia Mziwanda na Roman Mosha.
Alisema Tume ya uchunguzi iliyoundwa na serikali kuchunguza mgogoro huo ilibaini kuwa familia ya Tabia Mziwanda ambayo ilikuwa ikidai kuwa eneo hilo ni mali yao haikuwa nyaraka zozote zinazo halalisha umiliki wa eneo hilo.
Aliongeza kuwa Tume ilibaini Bwana Roman Mosha aliuziwa eneo lenye ukubwa ekari nne na kamati ya kijiji kwa kipindi hicho kinyume na taratibu za kuuza ardhi ya vijiji inayotaka uuzwaji wa ardhi uridhiwe kwenye Mkutano Mkuu wa Kijiji na si kamati.
‘’Bwana Mosha alileta mkataba wa mauziano ya ardhi baina yake na kijiji, ambayo inaonesha aliuziwa ekari nne, na katika kamati hiyo mmoja wao ni Mzee mziwanda ambae familia yake inadai kuwa eneo hilo ni mali yao, serikali imejiridhisha na ushahidi wote uliotolewa na kamati ya uchunguzi kuwa hakuwahi kuwa mmliki wa eneo hilo’’alisema.
Kheri alisema kuwa baada ya Serikali kushirikiki kamilifu katika kuchunguza mgogoro huo na kusikiliza pande zote mbili kihistoria, kimazingira, kinyaraka, viongozi wa Mtaa, na wazee wa Mtaa huo serikali imetoa maamuzi kuwa eneo hilo litabaki kuwa mali ya kijiji (mtaa),na kusimamiwa na Halmashauri ya Manispaa ya ubungo kama sheria ya ardhi inavyoelekeza.
Aliwataka viongozi wa Mitaa kuacha kuuza ardhi kiholela na badala yake kufuata taratibu za kuuza ardhi katika maeneo yao ili kuepusha migogoro mbalimbali ya ardhi inayojitiokeza na kuathiri shughuli mbalimbali za maendeleo.
’’Hakikisheni mnalilinda eneo hili, mtakapotaka kufanya matumizi mfuate taratibu, babu zetu walitenga maeneo haya kwaajili ya kupanua maendeleo ya mitaa kama vile kujenga shule, Vituo vya afya, na miradi mingine ya maendeleo hivyo yalindeni maeneo haya’’





0 Maoni