Zanzibar
Kiasi cha Shilingi
Bilioni Kumi na Tano na Milioni Mia mbili (15.2)kina hitajika kwaajili ya ujenzi
wa Mabweni ya Wanafunzi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere –
Kampasi ya Karume Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais
Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ameeleza hayo kupitia hotuba alioisoma kwa niaba ya
Rais Dk. Hussein Mwinyi katika hafla ya uwekaji wa Jiwe la Msingi la
mradi wa ujenzi wa Mabweni ya wanafunzi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu
Nyerere – Kampasi ya Karume Zanzibar, Bububu Mkoa wa Mjini Magharib .
Amesema ni vema wadau
wakaunga mkono juhudi za Serikali katika kuchangia Ujenzi wa Mabweni hayo ambao
yakikamilika yatasaidia wanafunzi kupata malazi bora na salama na hatimaye kupata
ari ya kusoma ili kupata maarifa bora yatakayoongeza maendeleo kwa Zanzibar na
Tanzania kwa ujumla.
Katika hatua nyengine
Mh Hemed amemwagiza mkandarasi anaetekeleza Mradi huo SUMA JKT kuhakikisha
mradi huo unajengwa katika ubora unaokubalika na kukamilika kwa wakati uliopangwa ili kutatua changamoto ya
Makaazi inayowakabili wanafunzi.
Amesema uwepo wa Chuo
cha kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere visiwani Zanzibar ni kielelezo
Chanya katika kuenzi na kudumisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa Vitendo.
Awali Waziri wa Elimu
na Mafunzo ya amali Zanzibar Mhe. Simai Mohamed Said amesema Wizara hiyo
itahakikisha inaendelea kushirikiana na chuo hicho huku ikizingatiwa kuwa
Wizara anayoingoza ipo katika mchakato wa kufanya marekebisho kupitia kitengo
chake kinachosimamia elimu ya juu ili kiweze kwenda sambamba na Wadau wa Elimu
Nchini.
Kwa upande wake Mkuu
wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Prof. Shadrack Mwakalila amesema Kampasi ya Karume imefanikiwa kutenga
fedha kupitia bajeti yake ikiwa na adhmna ya kutekeleza miradi mbali mbali
ikiwemo ujenzi wa Mabweni ya wanafunzi, Ujenzi wa madarasa ya kusomea, Ujenzi
wa Ofisi kwa upande wa Pemba pamoja na ujenzi wa nyumba za walimu.
Akisoma Taarifa ya
utekelezaji wa mradi huo Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la uzalishaji
Mali la jeshi la kujenga Taifa (SUMA-JKT) Kanali Absolonon Lyanga Shausi
alisema wanaishukuru serikali ya mapinduzi Zanzibar kupitia wakala wa majengo
Zanzibar kwa kuisajili SUMA-JKT kuweza kufanya kazi zake Zanzibar na kuahidi
kuwa mradi huo utakamilika ndani ya wakati uliopangwa wa kipindi cha miezi 18
huku ikizingatia weledi katika utekelezaji wake.




0 Maoni